Diamond ashtumiwa kusababisha Raila kushindwa kutwaa urais wa Kenya

Meneja wa zamani wa Diamond amedai kuwa kupiga picha naye ni ishara mbaya.

Muhtasari

•Meneja wa zamani wa Diamond, Ostaz Juma amedai kuwa sababu kuu ya mgombea urais huyo wa Azimio kushindwa ni kupiga picha naye.

•"Hujaibiwa. Wewe utamchukua aje Diamond kwenye shoo? Diamond saa hii ana gundu, watu hawamtaki, amekwisha," Ostaz alisema.

Mgombea urais Raila Oinga na staa wa Bongo Diiamond Platnumz
Image: EZEKIEL AMING'A

Staa wa Bongo Diamond Platnumz amedaiwa kusababisha Raila Odinga kushindwa kunyakua urais wa Kenya kwenye uchaguzi wa Agosti 9.

Meneja wake wa zamani Ostaz Juma Na Musoma amedai kuwa sababu kuu ya mgombea urais huyo wa Azimio kushindwa ni kupiga picha naye.

Kulingana na Ostaz, kupiga picha na bosi huyo wa WCB ni ishara mbaya na ni mwanzo wa masaibu katika maisha ya mtu.

"Nilipomuona Diamond kwenye shoo ya Raila, nilijishika kichwa nikasema mzee kaanguka. Mimi nilikuwa namkubali Raila, nilikuwa napenda sana awe rais wa Kenya. Lakini nilipomuona Diamond kwenye shoo yake nilijua amekwenda na maji," Ostaz Juma alisema katika mahojiano na Bongo Touch.

Meneja huyo wa muziki alipuuzilia mbali hatua ya Raila kpinga ushindi wa Ruto mahakamani akisisitiza kuwa kosa kubwa alilofanya ni kumwalika Diamond kutumbuiza katika mkutano wake wa mwisho wa kisiasa.

"Hujaibiwa. Wewe utamchukua aje Diamond kwenye shoo? Diamond saa hii ana gundu, watu hawamtaki, amekwisha," Alisema.

Ostaz alidai kuwa iwapo Raila angewaalika wasanii wengine wa Bongo kama Harmonize, Rayvanny ama Ali Kiba angetwaa urais.

"Raila ulichokibugi ni kumchukua Diamond. Ukipigwa picha naye umekwenda!" alidai.

Aliyekuwa meneja wa Diamond, Ostaz Juma Na Musoma
Image: HISANI

Diamond  alikuwa msanii mgeni maalum kwenye mkutano wa mwisho wa Azimio la Umoja-One Kenya mnamo Agosti 6.

Staa huyo alivuna takriban shilingi milioni 12 kwa kutumbuiza wafuasi wa Azimio kwa dakika chache ugani Kasarani.

Wakati wa shoo hiyo, Diamond alimpigia debe waziri huyo mkuu wa zamani  huku akisema  Kenya inamwaminia  kuwa rais.

"Nataka nikuambie vijana wanakuamini sana, nchi inakumaini sana, na wewe ndiye Rais unayefuata," Diamond alisema.

Kulingana na matokeo ya uchaguzi yaliyotangazwa na Wafula Chebukati mnamo Agosti 15, Raila aliibuka wa pili katika kinyang'anyiro cha urais cha mwaka huu huku William Ruto wa Kenya kwanza akinyakua kiti hicho.

Baada ya Ruto kutangazwa kama rais mteule Diamond Platnumz alituma salamu kwa Wakenya na kuwahimiza Wakenya kuungana na kufanya kazi pamoja kuenda mbele licha ya tofauti zao za kisiasa.

"Pongezi sana wana Kenya kwa kuhitimisha zoezi la uchaguzi na kumpata rais leo.. sasa hivi tena si Team Ruto, Wajackoyah ama Team Odinga, ni pamoja team Kenya ili kwa pamoja kuendeleza maendeleo ya Kenya na wana Kenya kwa ujumla," Bosi huyo wa WCB alisema kupitia ukurasa wake wa Instagram.