Hamisa Mobetto hatimaye afunguka kuhusu kutoka kimapenzi na Harmonize

Mpenziwe Hamisa, Kelvin alibainisha kuwa hata hamfahamu Harmonize wala hajawahi kumskia.

Muhtasari

•Hamisa alibainisha kuwa hakuna chochote kikubwa kati yake na Konde Boy na kubainisha kuwa mwimbaji huyo ni rafiki yake tu.

•Wakati alipoulizwa ikiwa anafahamu urafiki wa Harmonize na mpenzi wake, Kelvin aliweka wazi kuwa hata hamfahamu mwimbaji huyo.

amefunguka kuhusu uhusiano wake na Harmonize
Hamisa Mobetto amefunguka kuhusu uhusiano wake na Harmonize
Image: INSTAGRAM

Mwanamitindo wa Tanzania, Hamisa Mobetto amekana kuwahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi na bosi wa lebo ya Konde Music Worldwide, Harmonize.

Kwenye mahojiano na Rick Media, mpenzi huyo wa zamani wa Diamond Platnumz alibainisha kuwa hakuna chochote kikubwa kati yake na Konde Boy na kubainisha kuwa mwimbaji huyo wa kibao ‘Single Again’ ni rafiki yake tu.

“Yeye ni rafiki tu. Hakuna zaidi, hakuna kidogo, "alisema.

Baada ya kubainishiwa kuwa Harmonize anayapenda sana makalio yake makubwa, mama huyo wa watoto wawili alikiri kuwa hafahamu hilo.

Hamisa Mobetto alihojiwa baada ya kumpokea mpenzi wake wa sasa, Kelvin Sowax kutoka Togo nchini Tanzania wikendi iliyopita.

Wakati alipoulizwa ikiwa anafahamu urafiki wa Harmonize na mpenzi wake, Kelvin aliweka wazi kuwa hata hamfahamu mwimbaji huyo.

"Simjui, simjui," Kelvin alisema.

Hamisa alidokeza kuwa jamaa huyo kutoka Togo ambaye alimtangazia ulimwengu kama mpenzi wake mpya takriban mwezi mmoja uliopita hawafahamu marafiki zake wote.

Pia alisema kuwa mpenzi wake hajui chochote kuhusu Harmonize kuweka picha yake kama wallpaper kwenye simu yake.

“Atajuaje sasa... Sio jambo kubwa .." alisema.

Kelvin pia alithibitisha kuhusu kulipa mahari kwa mama huyo wa watoto wawili na kusema kuwa suala hilo ni kati yake na yeye.

Wiki iliyopita, Harmonize alimtambulisha aliyekuwa mpenzi wake, Hamisa Mobetto kama rafiki wake wa karibu almaarufu BFF.

Harmonize alianza kwa kupakia picha ya Hamisa Mobetto ambayo inamuonesha akiwa ameketi kwenye ndege, kwenye viwiko amepakata mto na viganjani ameshikilia simu kwa tabasamu akiwa kama anatumiana ujumbe na mtu.

“Kutana na BFF wangu mpya,” Harmonize aliandika.

Hamisa Mobetto naye si mchache. Aliichukua picha hiyo kutoka kwa Instastory ya Harmonize na kuichapisha kwenye ukurasa wake na kuandika “BFF” kisha kuiambatanisha na emoji za makopa ya mapenzi.