Akothee azungumzia kuolewa na mfanyibiashara maarufu baada ya kuonekana akitaniana naye

Siku ya Jumamosi, Akothee alisikika akitaniana na mfanyibiashara huyo kwa mzaha.

Muhtasari

•Akothee hivi majuzi alionekana akishiriki mlo na mshirika wake wa kibiashara wa muda mrefu, Mwenda Thuranira.

•Katika jibu lake, Akothee alibainisha kwamba yeye huwa hachumbii na mwanamume aliye kwenye ndoa tayari.

Image: HISANI

Mwimbaji na mjasiriamali Esther Akoth almaarufu Akothee hivi majuzi alionekana akishiriki mlo na mshirika wake wa kibiashara wa muda mrefu, Mwenda Thuranira.

Mama huyo wa watoto watano alichapisha baadhi ya picha na video za mkutano wake na mfanyabiashara huyo ambapo alisikika akitaniana naye kwa mzaha.

“Jamani, kutana na Mwenda wa 8. Kwa hiyo, nitakuwa Bi Mwenda, ah ah Thuranira the 8th,” Akothee alisikika akisema kwenye video hiyo huku akicheka.

Mwanamuziki huyo mwenye umri wa miaka 43 hata hivyo aliendelea kufafanua kuwa mkutano wake na Bw Thuranira ulikuwa kuhusu biashara tu.

"Tuko mkutano wa chakula cha mchana na biashara siku ya Jumamosi. Najua wengi wenu huwa mnasema, Jumamosi hapana,. Wafanyabiashara hatuna Jumamosi, hatuna Jumatatu, inabidi tufanye kazi,” alisema na kuendelea kuzungumzia baadhi ya uwekezaji wa Mwenda.

Mkutano kati ya wawili hao hata hivyo uliwaacha baadhi ya wanamtandao wakizungumza huku baadhi wakionekana kuchukulia kwa uzito utani wa Akothee kuhusu ‘Mwenda the 8th’.

Mtumiaji wa Facebook hata alijaribu kumshawishi mama huyo wa watoto watano kuolewa na Mwenda na kutaja baadhi ya faida za kuolewa katika jamii ya Wameru.

“Sasa fanya Thuranira awe wa 8 na uje Meru. Tunakupikia uji wa kijani ambao utakuwa ukiutamani kila siku,” Rodah Marangu alimwambia.

Katika jibu lake, Akothee alibainisha kwamba yeye huwa hachumbii na mwanamume aliye kwenye ndoa tayari.

"I don’t do married men,” alijibu.

Kumaanisha, “Sichumbiani na wanaume ambao wameoa.”

Image: FACEBOOK// AKOTHEE

Haya yanajiri wakati ambapo kuna tetesi nyingi kuwa ndoa ya mwimbaji huyo na Denis ‘Omosh’ Schweizer imekwisha na wawili hao hawapo pamoja tena.

Vitendo vya hivi majuzi kwenye mitandao vimezidisha tetesi za kuachana huku wanamitandao wakiwa na shauku kubwa ya kupata majibu.

Baadhi ya mambo ambayo yamewaacha watu wakizungumza ni Akothee kukiri hajakuwa sawa kisaikolojia katika miezi michache iliyopita, mwimbaji huyo kuacha kujitambulisha kama  ‘Bi Omosh’ kwenye Instagram na akaunti ya Omosh kuzimwa.

Akaunti ya Instagram ya Mister Omosh ilizimwa siku ya Jumatatu na kuzidisha uvumi kwamba kunaweza kuwa na matatizo fulani ambayo bado hayajafichuliwa. Akaunti hiyo ilikuwa na takriban wafuasi 72,000 kabla ya kutoweka. Hata hivyo, haijulikani ikiwa akaunti imezimwa kwa muda au kabisa.

Akothee tayari alikuwa ameacha kufollow akaunti hiyo kabla haijazimwa na pia alikuwa amefuta picha kadhaa za mume huyo wake mzungu.Mama huyo wa watoto watano pia alikuwa amefanya mabadiliko kadhaa kwenye akaunti yake ya Instagram, akiondoa jina 'Mrs Omosh' kutoka kwa wasifu wake.