Jamaa ajinyonga baada ya kusikiliza wimbo 'Dear Ex' wa Marioo kwa mara 60

“Jana Juma alikuja kwangu asubuhi, nilikaa naye akawa amefungua TV, akawa na muziki wake kauomba, huo muziki kaomba urudiwe mara 60 yaani wimbo huo huo," mwenyekiti alisema.

Muhtasari

• Mwenyekiti huyo alisema kwamba baada ya kama dakika 10 hivi, alifuatwa na majirani wa Juma wakimpa taarifa ya msiba wa kijana huyo.

Image: HISANI

Mwanamume mmoja mweney umri wa makamo katika mkoa wa Tanga nchini Tanzania ameripotiwa kufariki kwa kujinyonga baada ya kile kinakisiwa ni kutokana na wivu wa kimapenzi.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo ya kusikitisha iliyopeperushwa na runinga ya Wasafi, jamaa huyo aliyetambulika kwa jina Juma alifika nyumbani akiwa mwenye mawazo tele.

Aliingia kwa nyumba na akawa anaitazama runinga ambapo aliwaomba wenzake kumwekea wimbo wa Marioo, Dear Ex na kuutaka urudiwe kila mara hadi Zaidi ya mara 60.

“Chanzo tunavyohisi sisi ni mapenzi, alikuwa na mtu wake, na kweli wakapanga mambo yao mpaka kukaribia kumalizia lakini hapa kati kududu mtu akaingia na akavuruga, tunahisi hicho ndicho chanzo cha kujitoa uhai,” rafiki wa marehemu alinukuliwa na runinga hiyo.

Mwenyekiti wa kitongoji hicho alifichua kwamba alimuona Juma akisikiza wimbo huo kwa Zaidi ya mara 60 kabla ya kuondoka na baadae akapatikana amejitoa uhai.

“Jana Juma alikuja kwangu asubuhi, nilikaa naye akawa amefungua TV, akawa na muziki wake kauomba, huo muziki kaomba urudiwe mara 60 yaani wimbo huo huo, nakumbuka ni wimbo wa msanii aliyeimba ‘Dear Ex’, ilipofika saa nne mwanangu akataka kuangalia vibonzo lakini Juma akabisha akitaka bado kurudia ule muziki, nikamwambia umeshausikia, akashikwa na hasira akaondoka,” alisema Bi Mwanaid Abbas.

Mwenyekiti huyo alisema kwamba baada ya kama dakika 10 hivi, alifuatwa na majirani wa Juma wakimpa taarifa ya msiba wa kijana huyo.