Mulamwah hatimaye ahama kutoka bedsitter yake ya 9k, abeba mitungi na kamba za nguo

Mulamwah hatimaye amehama kutoka nyumba aina ya bedsitter ambayo amekuwa akiishi kwa miaka mingi.

Muhtasari

•Mulamwah alishiriki video ya vitu vyake vikisafirishwa kutoka nyumba hiyo iliyo katika mtaa wa Kariobangi hadi kwenye nyumba yake mpya.

•Mchekeshaji huyo alibainisha kuwa kuhama geto sio rahisi na akawahimiza watu kufanya kazi kwa bidii ili kupiga hatua.

Image: INSTAGRAM// MULAMWAH

Ilikuwa ni kipindi cha kujivunia wakati mchekeshaji David Oyando almaarufu Mulamwah hatimaye akihama kutoka nyumba aina ya bedsitter ambayo amekuwa akiishi kwa miaka mingi.

Baba huyo wa watoto wawili alitangaza hatua hiyo kubwa kupitia kurasa zake za mitandao ya kijamii mnamo siku ya Jumatano ambapo alishiriki video ya vitu vyake vikisafirishwa kutoka nyumba hiyo iliyo katika mtaa wa Kariobangi hadi kwenye nyumba yake mpya.

“Rasmi bana tumeondokea Ghetto bana. Ata wewe unaweza toka, weka bidii. Au sio?" Mulamwah alisema huku akiwaaga ambao walikuwa majirani zake.

Akiongea kwenye video ambayo alishiriki kwenye Instagram, mchekeshaji huyo alibainisha kuwa kuhama geto sio rahisi na akawahimiza watu kufanya kazi kwa bidii ili kupiga hatua.

Katika taarifa yake, alidokeza kuwa sasa anahamia kwenye nyumba ya vyumba vitatu vya kulala katika mtaa ambao hakufichua ambapo anataka mwanawe mdogo alelewe.

“Hatimaye !!... Mungu ni mkubwa KIJANA AMETOKA GHETO . Nitamiss bedsitter yangu ya 9k iliyonikaribisha mjini, marafiki zangu wa mtaa pia bana lakini tutapatana tu,” Mulamwah alisema.

Aliongeza, "Kulikuwa na misukosuko mingi lakini ilinisaidia sana kuokoa pesa na kuthamini maisha bora ♥️. Siku zote mshukuru na kumthamini MUNGU kwa hatua ndogo. Songa polepole, songa sawa."

Baba huyo wa watoto wawili pia alitumia fursa hiyo kuzungumzia jumba la kifahari analojenga nyumbani kwao Kitale akifichua kuwa linakaribia kukamilika.

“Wakati huo huo, wacha tuone maisha haya ya 3B ikoje kanairo. Ata sisi tuskie vile watu huskia bana . Kalamwah kaenjoy kidogo,” alisema.

"Mtu asikushow any , songa na pace yako ! tunahama hadi na mitungi na kamba za nguo 🤣 ladies give your men time 🙏💯,” aliongeza.

Hatua hii inajiri siku chache tu baada ya mchekeshaji huyo kumkaribisha mtoto wake wa kwanza na mpenzi wake wa sasa Ruth K.

Mapema mwezi huu, wawili hao walibarikiwa na mtoto wa kiume, Oyando Jr almaarufu Kalamwah ambaye ni mtoto wa pili wa Mulamwah. Ana mtoto mwingine na mpenzi wake wa zamani Carrol Sonie.