Njugush akejeli jirani Tanzania kwa kutopata medali yoyote katika Olimpiki ya Paris

Kenya tayari imeshapata medali kumi, lakini nchi jirani ya Tanzania bado haijapata hata shaba moja.

Muhtasari

•Njugush amefanya uchokozi wa kitani kwa Tanzania baada ya nchi hiyo jirani kuwa na matokeo mabaya katika  Olimpiki ya Paris.

•Kenya ndiyo nchi iliyofanya vyema zaidi Afrika katika Olimpiki ya Paris na ilishika nafasi ya 17 duniani kote kufikia Jumamosi.

Image: INSTAGRAM// NJUGUSH

Mchekeshaji maarufu wa Kenya Timothy Kimani almaarufu Njugush amefanya uchokozi wa kitani kwa Tanzania baada ya nchi hiyo jirani kuwa na matokeo mabaya katika mashindano ya Olimpiki ya Paris yanayokaribia kuisha.

Shindano hilo lililoanza kuelekea mwishoni mwa mwezi uliopita litafikia tamati leo Jumapili Agosti 11, huku fainali mbalimbali zikifanyika mchana kabla ya kufungwa rasmi baadaye jioni.

Kenya tayari imeshapata medali kumi tangu kuanza kwa mashindano hayo, lakini nchi jirani ya Tanzania bado haijapata hata shaba moja, jambo ambalo Njugush ametumia kuwakejeli.

"Majirani jamani kimya kingi utajenga ukuta.. Hata bronzi nyie kwani shi ngaa??.. ama mna mwendo kasi?," Njugush aliandika kwenye Instagram.

Mchekeshaji huyo aliweka wazi kuwa hata hivyo hana vita na majirani hao na kubainisha kuwa licha ya kutofanya vizuri kwenye michuano ya Olimpiki, bado wanafanya vizuri kwenye muziki.  

“Jamani majirani sina ubaya yakhe.. kwanza pale France Komasava ingenogaa,” alisema.

Tazama maoni ya baadhi ya wanamtandao waliojibu chapisho hilo;

Car10cs: Wako darassani wakiharmonize rays zao ndo wang’are na ma diamond wakizichukulia kwa mali ya akiba.

Kalondu_musyimi: Wewe ni mchokozi.

Creative_savage3.0: Wakenya mko na magold lakini bado mnawaza Jirani,, wakati jirani hawazi kitu anyway, angukeni nayo.

Mashirima_kapombe: Mchokozii

Telehmani: Wako sawa na diamond platnumz.

Hadi kufikia Agosti 10, China iliongoza kwa medali 90 (dhahabu 39, fedha 27 na shaba 24), ikifuatiwa na Marekani yenye jumla ya medali 122 (dhahabu 38, fedha 42 na shaba 42), na Australia yenye medali 50. .

Kenya ndiyo nchi iliyofanya vyema zaidi barani Afrika katika Michezo ya Olimpiki ya Paris na ilishika nafasi ya 17 duniani kote kufikia Jumamosi. Tayari timu ya Kenya imeshinda dhahabu 4, fedha 2 na shaba 4.