"Diamond akitaka kunirudia, anaweza kurudi!" Zari atangaza huku akitishia kumuacha mumewe Shakib

“Mpenzi, ikiwa hunitambui mimi ni nani, kwa bahati mbaya nitapata mtu wa kuchukua nafasi yako. Na siogopi," Zari alimwambia mumewe.

Muhtasari

•Zari alifichua kuwa mumewe hana uhakika kuhusu ndoa yao na amekuwa akihoji uhusiano kati yake na mzazi mwenzake, Diamond Platnumz.

•"Ikiwa mtu wangu hataki kunitambua mimi ni nani, aibu. Hakika nitapata mtu ambaye atatambua thamani yangu," Zari alisema.

Zari Hassan, D Voice na Diamond Platnumz
Image: HISANI

Sosholaiti na mfanyibiashara wa Uganda Zari Hassan ametishia kuvunja ndoa yake na mumewe Shakib Cham Lutaaya iwapo kijana huyo mwenye umri wa miaka 31 hatabadilika.

Katika kipindi cha moja kwa moja kwenye akaunti yake ya mtandao wa kijamii, mama huyo wa watoto watano alifichua kuwa mumewe hana uhakika kuhusu ndoa yao na amekuwa akihoji uhusiano kati yake na mzazi mwenzake, Diamond Platnumz.

Zari alisema alilazimika kufanya kipindi cha moja kwa moja ili kueleza wazi kuwa yeye na Diamond hawako kwenye uhusiano wowote wa kimapenzi, ili tu kumhakikishia mumewe kuhusu auaminifu wake katika ndoa yao

“Ngoja niwaambie kitu, Nikitaka kumrudia Diamond naweza kurudi. Ikiwa Diamond anataka kunirudia, anaweza kurudi. Lakini sisi tumemalizana. Sisi tumemalizana kabisa. Simtaki, hanitaki,” Zari alisema Jumapili usiku.

Sosholaiti huyo aliweka wazi kuwa ana mume na mzazi mwenzake pia ana mpenzi.

“Mume wangu hajiamini sana, na hilo linaleta matatizo mengi. Lazima niwe hapa kuelezea. Kweli? Boss lady mzima, inabidi nifanye kipindi chote cha moja kwa moja, ili tu kuthibitisha uhakika kwa mume wangu. Kipindi hiki ni kuthibitisha kitu kwa mume wangu,” aliongeza.

Mfanyabiashara huyo mwenye umri wa miaka 43 alibainisha kuwa ana sifa zote nzuri na anaweza kuwa na mtu yeyote ambaye anataka kuwa naye.

"Lakini nilimchagua mume wangu, na sijali jinsi nyinyi mnamwona. Ooh, amefilisika, hafai vya kutosha, sijali. Nilimchagua. Nilichagua kuwa naye kama mume wangu, kisha ananiweka katika hili!!,” alisema.

Zari alidokeza kuwa mumewe hana budi kuacha kutokuwa na uhakika kuhusu ndoa yao ikiwa anataka iendelee vyema.

Aidha, alijigamba kwamba anaweza kupata mtu mwingine wa kuchukua nafasi ya mfanyibiashara huyo wa Uganda ikiwa hamwamini.

"Afadhali jamaa wangu abadilike, bora atambue hili. Ikiwa mtu wangu hataki kunitambua mimi ni nani, aibu. Hakika nitapata mtu ambaye atatambua thamani yangu kwa sababu nina thamani zaidi,” alisema.

“Mpenzi, ikiwa hunitambui mimi ni nani, kwa bahati mbaya nitapata mtu wa kuchukua nafasi yako. Na siogopi,"

Alibainisha wazi kwamba yeye ni mwaminifu kila wakati kwa mtu ambaye anachumbiana kwa wakati mmoja.

Drama zote kwenye ndoa ya Zari zilianza siku chache zilizopita wakati mwimbaji Diamond alipomtembelea sosholaiti huyo nchini Afrika Kusini kusherehekea siku ya kuzaliwa ya binti yao Latiffah Daongote.