Zari azungumzia alivyokuwa mke mwema kwa Shakib kabla ya ndoa yao kusuasua

"Wakati mwingine shinikizo huwa kubwa na kusababisha vitu fulani kulipuka kama volcano. Kuna sababu nyuma ya kila kitu,” Zari alisema.

Muhtasari

•Mrembo huyo mwenye alifichua kuwa kuna sababu nyuma ya kila kitu kilichotokea katika siku za hivi majuzi.

•"Nilipenda, nilijisalimisha, nilikuwa mwenye heshima, nilikuwa mwaminifu, nilikuwa wa kweli, nilijali, nililea," alisema.

Image: INSTAGRAM// SHAKIB CHAM

Sosholaiti mashuhuri wa Uganda Zari Hassan ameendelea kudokeza kuwa mambo si mazuri katika ndoa yake na mfanyabiashara Shakib Cham Lutaaya.

Katika taarifa kwenye akaunti yake ya Snapchat siku ya Jumanne, mrembo huyo mwenye umri wa miaka 43 alifichua kuwa kuna sababu nyuma ya kila kitu kilichotokea katika siku za hivi majuzi.

Alibainisha kuwa wakati mwingine mambo yanayofanyika kwa usiri huongezeka hadi kufikia hatua ya kulipuka na kufichuka wazi.

"Wakati mwingine shinikizo huwa kubwa na husababisha vitu fulani kulipuka kama volcano. Kuna sababu nyuma ya kila kitu,” Zari alisema.

Mama huyo wa watoto watano aliendelea kuorodhesha sifa zake kama mpenzi wakati akiwa kwenye ndoa  kabla mambo hayageuka kuwa mabaya hivi majuzi.

Alizungumza kuhusu jinsi alivyokuwa mwaminifu, mwenye heshima na mkweli kwa mpenziwe huyo mwenye umri wa miaka 31, akibainisha kwamba alikuwa mke mzuri.

"Nilipenda, nilijisalimisha, nilikuwa mwenye heshima, nilikuwa mwaminifu, nilikuwa wa kweli, nilijali, nililea," alisema.

Haya yanajiri siku moja tu baada ya sosholaiti huyo mrembo kuzamia kwenye mitandao ya kijamii kumzomea mumewe Shakib na kutishia kumuacha.

Katika kipindi cha moja kwa moja kwenye akaunti yake ya mtandao wa kijamii, mama huyo wa watoto watano alifichua kuwa mumewe hana uhakika kuhusu ndoa yao na amekuwa akihoji uhusiano kati yake na mzazi mwenzake, Diamond Platnumz.

Zari alisema alilazimika kufanya kipindi cha moja kwa moja ili kueleza wazi kuwa yeye na Diamond hawako kwenye uhusiano wowote wa kimapenzi, ili tu kumhakikishia mumewe kuhusu auaminifu wake katika ndoa yao

“Ngoja niwaambie kitu, Nikitaka kumrudia Diamond naweza kurudi. Ikiwa Diamond anataka kunirudia, anaweza kurudi. Lakini sisi tumemalizana. Sisi tumemalizana kabisa. Simtaki, hanitaki,” Zari alisema Jumapili usiku.

Sosholaiti huyo aliweka wazi kuwa ana mume na mzazi mwenzake pia ana mpenzi.

“Mume wangu hajiamini sana, na hilo linaleta matatizo mengi. Lazima niwe hapa kuelezea. Kweli? Boss lady mzima, inabidi nifanye kipindi chote cha moja kwa moja, ili tu kuthibitisha uhakika kwa mume wangu. Kipindi hiki ni kuthibitisha kitu kwa mume wangu,” aliongeza.

Mfanyabiashara huyo mwenye umri wa miaka 43 alibainisha kuwa ana sifa zote nzuri na anaweza kuwa na mtu yeyote ambaye anataka kuwa naye.

"Lakini nilimchagua mume wangu, na sijali jinsi nyinyi mnamwona. Ooh, amefilisika, hafai vya kutosha, sijali. Nilimchagua. Nilichagua kuwa naye kama mume wangu, kisha ananiweka katika hili!!,” alisema.

Zari alidokeza kuwa mumewe hana budi kuacha kutokuwa na uhakika kuhusu ndoa yao ikiwa anataka iendelee vyema.