Harmonize aweka mambo bayana kuhusu kuhuzunika, kugeukia pombe kwa sababu ya Kajala

Konde Boy alisema kuwa wapenzi wake wote wa zamani ni marafiki zake.

Muhtasari

•Konde Boy alikana kuzama katika ulevi kwa sababu ya kuandamwa na mawazo ya mpenzi wake wa zamani.

•Alisema yeye ni rafiki wa yeyote ambaye amewahi kuchumbiana naye au kuwa na uhusiano wa kimapenzi naye.

Harmonize na aliyekuwa mchumba wake Kajala Masanja
Image: INSTAGRAM// HARMONIZE

Staa wa Bongo, Rajab Abdul Kahali almaarufu Harmonize amekanusha madai ya kukumbwa na msongo wa mawazo kwa sababu ya mpenzi wake wa zamani.

Katika taarifa kwenye ukurasa wake wa Instagram, bosi huyo wa Konde Music Worldwide pia alikana kuzama katika ulevi kwa sababu ya kuandamwa na mawazo ya mpenzi wake wa zamani.

Konde Boy alisema kuwa wapenzi wake wote wa zamani ni marafiki zake na akabainisha kuwa hakuna hata mmoja wao anayeweza kumfanya azame kwenye ulevi.

"Wakati mwingine kuonja mtungi kidogo sio mbaya!! Ni burudani. Nimeongea hivi kwa sababu nishaanza kuona comment za wajuajii. OOOH, sijuwi anakunywa sanaa ana mawazo ya mapenzi!! Kwa X gani.. X zangu wote ni washikaji zangu. Ni swala la maamuzi tuu nirudi wapi!! Wakunifanyia nilewe chakali hayupo!!Sijalewa na sitokuja kulewa,” Harmonize aliandika kwenye Instastori siku ya Jumatano jioni.

Baba huyo wa binti mmoja alisema kwamba yeye ni rafiki wa mwanamke yeyote ambaye amewahi kuchumbiana naye au kuwa na uhusiano wa kimapenzi naye.

Kuthibitisha kauli yake, mwanamuziki huyo alichapisha screenshot ya gumzo lake la video na mmoja wa mpenzi wake wa zamani, Sarah Michelloti na kufichua kwamba kwavkawaida huwa wanazungumza na kushiriki hadithi mara kwa mara.

“Imagine Sara ni mwanangu na tunapigaga stori. Sasa kitu gani? Au X vipi? Wakunifanyia ninywe nilewe? Ma X zangu wote ni wanangu!! Some times naamua tu kuchangamsha Instagram,” aliandika Konde Boy.

Aliongeza, “Sina kinyongo na yeyote tulie wahi kushare kitanda kimoja na ninawaambieni. Kwenye kazi zao na mahusiano yaoo!! Sinywi kupitiliza. Najipongezaga tuu. Maneno hapa nishapiga zangu glasi za wine baada ya chakula. Sijalewa hata.”

Image: INSTAGRAM// HARMONIZE

Staa huyo wa bongo fleva alibainisha kwamba huwa hapigi maji kwa sababu ya msongo wa mawazo ya mwanamke bali anakunywa champagne kidogo ili kusaidia katika kusaga chakula.

Kwa muda mrefu, kumekuwa na madai kuwa mwimbaji huyo mwenye umri wa miaka 30 aliathiriwa vibaya na kutengana kwake na muigizaji Frida Kajala Masanja mwishoni mwa mwaka jana hadi kufikia hatua ya yeye kutafuta faraja kwa pombe, madai ambayo sasa anayakanusha.

Miezi michache iliyopita, Konde Boy aliahidi kufichua mambo mengi kuhusu mahusiano yake yaliyovunjika  na mama huyo  wa binti mmoja  baada ya kulewa, jambo ambalo alilifanya na kuibua vita vingi vya maneno kati yao kwenye mitandao ya kijamii na vyombo vya habari.