•Jumatatu asubuhi mfanyibiashara huyo alizua wasiwasi mitandaoni baada ya kufichua kuwa alilazwa hospitalini baada ya kuugua ghafla.
•Jimal sasa amesema kuwa afya yake tayari imerejea kikamilifu na kufichua kuwa ameruhusiwa kutoka hospitalini.
Mwenyekiti wa Muungano wa Wamiliki Matatu jijini Nairobi Jimal Marlow Rohosafi ameweka wazi kuwa sasa yupo sawa baada ya kuugua mapema wiki hii.
Jumatatu asubuhi mfanyibiashara huyo alizua wasiwasi mitandaoni baada ya kufichua kuwa alilazwa hospitalini baada ya kuugua ghafla.
Jimal alieleza kwamba alishambuliwa na ugonjwa usiothibitishwa muda mfupi tu baada ya kuondoka kazini Jumapili usiku.
"Nachukia hospitali.. sekunde chache tu baada ya kutoka ofisini.. Nilihisi kuwa siko sawa, kila kitu kitakuwa sawa," Jimal alitangaza Jumatatu asubuhi kupitia ukurasa wake wa Instagram.
Baba huyo wa watoto wawili aliambatanisha ujumbe wake na picha iliyoonyesha akiwa amelala kwenye kitanda cha hospitali na kudokeza kuwa alilazwa mwendo wa saa saba usiku wa kuamkia Jumatatu.
Hata hivyo hakutoa maelezo zaidi wala kufichua ugonjwa ambao ulimuathiri hadi kufikia hatua ya kulazwa.
Jimal sasa amesema kuwa afya yake tayari imerejea kikamilifu na kufichua kuwa ameruhusiwa kutoka hospitalini.
"Alhamdullah.. Nipo sawa sasa. Shukran nyote kwa kunijulia hali. Sasa tupo site!" Jimal alitangaza Jumanne kupitia Instastori zake.
Mfanyibiashara huyo pia alipakia picha zake kadhaa za sasa zilizoonyesha akiwa mchangamfu na buheri wa afya.
"Sio kila wakati kuhusu mali !! Baadhi ya watu wanaona wivu juu ya utu wako, nguvu zako na jinsi watu wengine wanavyokupenda.. 100% afya nzuri, afya ni mali, tabasamu zaidi," Aliandika chini ya picha alizopakia.
Jimal amezungumziwa sana mitandaoni katika kipindi cha takriban mwaka mmoja ambacho kimepita huku wanamitandao wakiangazia ndoa yake.
Wiki kadhaa zilizopita mfanyibiashara huyo alipiga hatua ya kuomba msamaha kutoka kwa mkewe kwa kualika drama nyingi kwenye ndoa yao ya miaka mingi.
Ndoa ya Jimal ilianza kusambaratika mwaka jana baada ya kujitosa kwenye mahusiano na mwanasoshalaiti Amber Ray.
Amber Ray kwa sasa yupo kwenye mahusiano mengine huku Jimal akihangaika kumrejesha nyumbani mkewe Amira.