"Tukutane mahakamani!" Akothee atoa onyo kali kwa wanablogu, ataka kulipwa milioni 300

"Fahamishwa kuwa jina la Akothee limejengwa kwa miaka kadhaa kwa kujitolea sana na bidii," alionya.

Muhtasari

•Akothee aliwashutumu wanablogu kwa kuchapisha taarifa za kupotosha kumhusu kwenye mitandao ya kijamii.

•Alionya kwamba wale ambao hawatatii onyo lake wanahatarisha kukabiliwa na mashtaka ambayo yatavutia fidia kubwa ya uharibifu ya hadi shilingi 300,000,000.

Image: INSTAGRAM// AKOTHEE

Mwimbaji mashuhuri Esther Akoth almaarufu Akothee ametishia kuwashtaki wanablogu na wanavlogu Wakenya kwa kumharibia jina.

Katika taarifa ya umma ambayo alitoa siku ya Jumanne, mama huyo wa watoto watano aliwashutumu waandishi na watayarishi kwa kuchapisha taarifa za kupotosha kumhusu kwenye mitandao ya kijamii.

Alidai kuwa wanaochapisha ripoti hizo wanafanya kimakusudi kwa lengo la kusambaza habari za kupotosha na za uwongo.

"Fahamishwa kuwa jina la Akothee limejengwa kwa miaka kadhaa kwa kujitolea sana na bidii," alionya katika taarifa hiyo.

"Aliongeza "Ilani hii limetolewa kwa wanablogu na wanablogu wote wanaoendelea kuchapisha blogu na vlogu potofu na za uwongo pamoja na matamshi ya kashfa kutokana na nia mbaya dhidi ya jina la Akothee."

Mjasiriamali huyo mwenye umri wa miaka 42 alionya kwamba wale ambao hawatatii onyo lake wanahatarisha kukabiliwa na mashtaka ambayo yatavutia fidia kubwa ya uharibifu ya hadi shilingi 300,000,000.

"Mtalazimika kuniomba ruhusa ya  kuchapisha habari za jina langu kwenye kurasa zenu. Tukutane mahakamani au mnihisi moja kwa moja kwenye mifuko yenu. Hatuna wanablogu nchini Kenya, tuna wanyanyasaji wa mtandaoni na wauaji wa wahusika. Sio mimi, " alisema kupitia ukurasa wake wa Instagram.

Siku za hivi majuzi, Akothee amekuwa akivuma sana kwenye mitandao ya kijamii hasa baada ya kumtambulisha mpenzi wake mzungu, Bw Omondi, miezi michache iliyopita. Mwanamuziki huyo alimtambulisha Bw Omondi miezi kadhaa baada ya kutangaza kutengana  na aliyekuwa meneja wake Nelly Oaks.