"Yuko huru kufanya chochote" Zuchu amkana Diamond kuwa mpenziwe baada ya sakata ya Tanasha

Zuchu alibainisha kuwa Diamond si mpenzi wake kwani hajakuwa kwenye mahusiano kwa muda sasa.

Muhtasari

• Zuchu kwa mara nyingine amelazimika kujitokeza na kufafanua uhusiano wake na bosi wa WCB, Diamond Platnumz.

•“Sio bwanangu mpenzi. Nimekuwa single kwa muda sasa hivyo yuko huru kufanya chochote anachotaka,” Zuchu alijibu.

katika ziara yao ya Ufaransa.
Diamond Platnumza na anayedaiwa kuwa mpenziwe, Zuchu katika ziara yao ya Ufaransa.
Image: INSTAGRAM// ZUCHU

Malkia wa Bongo fleva, Zuhura Othman almaarufu Zuchu kwa mara nyingine amelazimika kujitokeza na kufafanua uhusiano wake na bosi wa WCB, Diamond Platnumz.

Huku gumzo kubwa ambalo linawahusisha yeye, Diamond, Tanasha Donna na Mama Dangote likiendelea, msanii huyo mzaliwa wa Zanzibar ameibuka na kumkana bosi huyo wa WCB kama mume wake baada ya shabiki kumuuliza iwapo anafahamu kuhusu hatua ya Tanasha ya hivi majuzi.

“Umemuona bwana ako na Tanasha Jana wavuvi wamenoga htri,” mtumizi wa Instagram alimwandikia Zuchu kwenye sehemu ya maoni ya chapisho lake.

Katika majibu yake, mwimbaji huyo wa kibao ‘Sukari’ alibainisha kuwa Diamond si mpenzi wake kwani hajakuwa kwenye mahusiano kwa muda sasa.

Binti huyo wa Khadija Kopa aliongeza kuwa bosi wake sasa yuko huru kufanya lolote analotaka kufanya kwani hawana mahusiano ya kimapenzi.

“Sio bwanangu mpenzi. Nimekuwa single kwa muda sasa hivyo yuko huru kufanya chochote anachotaka,” Zuchu alijibu.

Haya yanajiri wakati ambapo kumekuwa na wasiwasi mkubwa kuhusu nafasi yake ya sasa katika maisha ya Diamond baada ya Tanasha kupongezwa na Mama Dangote kwa kumzawadia zawadi za gharama kubwa.

Mamake Diamond pia alidaiwa kugombana na msanii huyo wa kike wa WCB na hata kudaiwa kumblock kwenye mtandao wa Instagram, madai ambayo tayari ameyakanusha.

Siku ya Alhamisi, Mama Dangote alikanusha madai ya kugombana na Zuchu ambayo yalikuwa yakisambaa mitandaoni.

Tetesi za mzozo kati ya Mama Dangote na Zuchu ziliibuka Alhamisi baada ya mama huyo wa Diamond kudaiwa kum-unfollow malkia huyo wa bongo fleva kwenye mtandao wa Instagram. Pia alidaiwa kukubaliana na maoni ya shabiki mmoja aliyependekeza Diamond kurudiana na Tanasha na kumtimua Zuchu.

Wakati akijibu tuhuma hizo, Mama Dangote aliweka wazi kuwa hajamfuata wala kum-unfollow mtu yeyote kwenye Instagram hivi majuzi.

“Mimi wasije wakaniingiza kwenye mambo yao. Mimi sijamu-unfollow. Niliowa-follow hao hamsini, ndio hao hao hamsini. Sasa nimuunfollow kwa kipi?” Mama Dangote aliiambia Wasafi Media.

Aliongeza, “Mimi mwenyewe ata nikigombana na mtu atajua mwenyewe. Niliowa-follow ni hao hamsini ,sina hamsini na moja. Mambo ya kitoto ya zamani wasiniingize. Mimi najijua mtu mzima. Mimi nimuunfollow amenifanya nini?”

Mamake Diamond aliwasihi watu kutomuingiza kwenye ugomvi na Zuchu huku akimtaja malkia wa Zanzibar kama bintiye.

“Wasinigombanishe na mwanangu Zuchu. Mimi sina ugomvi na mtu. Wasiniingize kwenye mambo hayo,” alisema.