Zaheer Jhanda, Mbunge aliyekuwa mumewe Amber Ray ataka bidhaa za urembo kuongezwa ushuru

Amber Ray alikuwa mke wa pili wa mbunge huyo kwa miaka mitatu.

Muhtasari

•Zaheer ambaye ni mume wa zamani wa mwanasoshalaiti maarufu Amber Ray alisema ushuru wa bidhaa kama vile vipondozi, wigi na kope bandia unafaa kuongezwa.

•Alisema imefika wakati wanawake wajifunze kuwa natural akibainisha kuwa "hao wamama wametusumbua sana,"

Mbunga Zaheer Jhanda
Image: FACEBOOK

Mbunge wa Nyaribari Chache Zaheer Merlahi Jhanda  ameapa kuwasilisha muswada bungeni kutaka kuongezwa kwa ushuru wa bidhaa za urembo.

Siku ya Alhamisi akizungumza na waandishi wa habari nje ya bunge, Zaheer ambaye ni mume wa zamani wa mwanasoshalaiti maarufu Amber Ray alisema ushuru wa bidhaa kama vile vipondozi, wigi na kope bandia unafaa kuongezwa.

"Nitahakikisha muswada huo nimeusukuma na hiyo bei iongezeke ile tuweze kuchukua ushuru kutoka kwa akina mama hao," alisema.

Zaheer alisema wanawake hawapaswi kulalamika kuhusu ongezeko la bei ya bidhaa za urembo na kubainisha kuwa wanaume ndio huwapatia pesa za kuzinunua.

"Hilo suala la make up, watajua hawajui. Huo muswada lazima upitishwe bungeni," alisema.

Mbunge huyo alibainisha kuwa serikali inatakiwa kutafuta mbinu za kuongeza mapato ya kodi ikiwa ni pamoja na kuzitoza bidhaa za urembo ushuru.

Alisema imefika wakati wanawake wajifunze kuwa natural akibainisha kuwa "hao wamama wametusumbua sana,"

"Hao wanadada ndio wanatumia hizi viti. Nataka ushuru upandishwe 100% katika bidhaa kama vipondozi. Hawa watu wametusumbua sana," alisema.

Zaheer alichaguliwa kuwa mbunge wa Nyaribari Chache katika uchaguzi wa Agosti 9 kwa tiketi ya chama cha UDA. Alimridhi aliyekuwa mbunge Richard Nyagaka Tongi.

Mfanyibiashara huyo aliwahi kuwa kwenye ndoa na mwanasoshalaiti asiyepungukiwa na drama, Amber Ray. Wawili hao walikuwa pamoja kwa kipindi cha takriban miaka mitatu kabla ya kutengana katika hali tatanishi.

Amber Ray alikuwa ameolewa kama mke wa pili wa mwanasiasa huyo.