Diamond Platnumz ajigamba kuhusu mwanawe na Tanasha Donna kufuatia fanikio kubwa shuleni

Naseeb Junior mnamo Ijumaa alitambuliwa kama ‘Nyota wa Wiki’ na shule ya kifhari anakosomea na kutunukiwa cheti.

Muhtasari

•Naseeb alitunukiwa cheti kwa kutulia vizuri katika shule yake mpya kwa kujiamini na kuanza kuelewa utaratibu na shughuli za kila siku.

•Naseeb Junior ambaye ni mwanawe Diamond na Tanasha Donna alianza safari yake ya kusoma nchini Tanzania mapema mwezi huu..

Naseeb Jr amemfanya baba yake Diamond Platnumz ajivunie
Image: HISANI

Staa wa Bongo Naseeb Adul Juma almaarufu Diamond Platnumz alishindwa kuficha furaha yake kufuatia ushindi mkubwa wa mwanawe Naseeb Juniour shuleni hivi majuzi.

Takriban wiki mbili tu baada ya kujiunga na Shule ya Kimataifa ya Braeburn Dar es Salaam nchini Tanzania, Naseeb Junior mnamo siku ya Ijumaa alitambuliwa kama ‘Nyota wa Wiki’ na shule hiyo ya kifhari na kutunukiwa cheti.

Mafanikio hayo makubwa yalimfanya mwanamuziki Diamond Platnumz kuwa baba mwenye fahari na akashiriki habari hizo njema pamoja na mashabiki wake kwenye mitandao ya kijamii.

“Mwanangu @naseeb.junior ananifanya nijivunie shuleni #StarOfTheWeek,” Diamond aliandika kwenye picha ya cheti cha Naseeb Jr aliyoweka kwenye ukurasa wake wa Instagram.

Kulingana na maelezo kwenye cheti hicho, mvulana huyo mwenye umri wa miaka minne alitunukiwa cheti hicho kwa kutulia vizuri katika shule yake mpya kwa kujiamini na kuanza kuelewa utaratibu na shughuli za kila siku.

“Anafika shuleni kwa furaha na kuwasalimia walimu wake, kisha anatafuta midoli anayopenda kucheza nayo (nyani). Natarajia kumuona Nasibu akiendelea zaidi na kujengea ujasiri katika nyanja zote za masomo yake. Umefanya vizuri,” yalisomeka maelezo kwenye cheti.

Mafanikio hayo yalimfanya Diamond kumsherehekea mtoto huyo wake wa mwisho kama staa.

Image: INSTAGRAM// DIAMOND PLATNUMZ

Naseeb Junior ambaye ni mwanawe Diamond na Tanasha Donna alianza safari yake ya kusoma nchini Tanzania mapema mwezi huu..

Mvulana huyo ambaye anatajwa kuwa ndiye pendwa Zaidi kati ya watoto wanne wa Diamond kwa muda sasa amekuwa akionekana na nyanya yake, Mama Dangote na ilifichuliwa hatimaye waliamua kumuanzishia elimu yake ya msingi nchini Tanzania

Katika video ambayo Mama Dangote alipakia kwenye ukurasa wake wa Instagram takriban wiki mbili zilizopita, Naseeb Jr alionekana amevalia sare za shule katika baraza la shule ya kifahari huku akiwa anadeka.

Mama Dangote aliandika kwamba Diamond Platnumz ndiye alirauka alfajiri mapema kumpeleka mwanawe shule, akionesha furaha kwamba mrithi wa mwanawe naye ameanza safari ya kuyabukua mabuku.

“Kweli Tom kaka amekuwa.. Atimae Naseeb kichwa @diamondplatnumz 🦁 anaamka asubuhi kumpeleka mtoto @naseeb.junior shule… 🤲” aliandika Mama Dangote.

Kwa mujibu wa blogu moja kutoka nchini humo ambaye ilidai kwamba shule ya Naseeb Jr  ipo katika maeneo ya karibu na ofisi zao, walifichua kuwa karo ya kumuingiza mtoto kama Naseeb Jr si chini ya shilingi milioni 40 za Kitanzania.

Blogu hiyo ilisema kwamba shule hiyo iko katika maeneo ya Mbezi Beach na kama si kuongoza kwa gharama ya juu ya karo basi ni miongoni mwa shule zenye gharama ya thamani iliyotukuka.