Hamisa Mobetto achoka kujaribu mahusiano, aomba Kevin awe mume wake wa maisha

Mwanamitindo huyo amefanya maombi maalum kwa Mungu akitaka Kevin awe mwanamume wa mwisho kuchumbiana naye.

Muhtasari

•Mpenzi huyo wa zamani wa mwimbaji Diamond Platnumz alidokeza kuwa amechoka kujaribu mahusiano mapya mara kwa mara.

“Siku moja nitatambulishwa kama “mke mrembo” simama usalimie watu. Nitasimama kwa masaa matano bila kuchoka,” alisema Hamisa.

na mpenzi wake Kevin.
Hamisa Mobetto na mpenzi wake Kevin.
Image: INSTAGRAM// HAMISA MOBETTO

Mwanasosholaiti na mwanamitindo maarufu wa Tanzania Hamisa Mobetto ameonekana kuridhishwa sana na mpenzi wake wa sasa Kevin Sowax kuwa mshirika wake wa maisha.

Katika taarifa fupi siku ya Jumanne, mpenzi huyo wa zamani wa mwimbaji Diamond Platnumz alidokeza kuwa amechoka kujaribu mahusiano mapya mara kwa mara.

Kutokana na hilo, Hamisa sasa amefanya maombi maalum kwa Mungu akitaka Kevin awe mwanamume wa mwisho kuchumbiana naye huku akitumai kwamba uhusiano wao utapelekea ndoa.

“Namuomba Mungu wa Mwisho awe ni wewe @kevinsowax,” Hamisa aliandika chini ya picha zake na Mtogo huyo ambazo alichapisha kwenye Instagram.

Kuambatana na picha alizochapisha, pia alishiriki meme akiashiria jinsi anavyotaka sana kuwa katika ndoa thabiti siku moja.

“Siku moja nitatambulishwa kama “mke mrembo” simama usalimie watu. Nitasimama kwa masaa matano bila kuchoka,” meme hiyo ilisoma.

Kevin ambaye kwa sasa yuko Tanzania kwa ziara yake ya kwanza katika nchi hiyo ya wakwe zake pia alichapisha picha zake na mwanamitindo huyo na kwenye sehemu ya maelezo akasema, “Nguvu ya mapenzi @hamisamobetto.

Mwanaume huyo Mtogo aliwasili katika nchi hiyo jirani usiku wa kuamkia siku ya Jumatatu na Hamisa Mobetto alimkaribisha na maua kabla ya wawili hao kuwa na mazungumzo na waandishi wa habari.

Katika mahojiano, Kevin alibainisha kuwa yupo nchini Tanzania kwa ajili ya mpenzi wake Hamisa. Pia alifichua atakutana na watoto wa mwanamitindo huyo, Fantasy Majizzo na Dylan Abdul Naseeb kwa mara ya kwanza.

"Itakuwa mara ya kwanza kukutana nao na siwezi kusubiri. Huwa tunazungumza kupitia simu, kupitia video ya simu. Tutakutana ana kwa ana kwa mara ya kwanza,” Kelvin alisema.

Kelvin alifichua kuwa yeye binafsi hana watoto lakini akadokeza kuwa anasubiri kwa hamu kupata watoto kadaa na Hamisa.

"Siwezi kusubiri," alisema.

Mtogo huyo aidha alifichua kuwa alikutana na Hamisa katika hafla ya faragha nchini China na akavutiwa naye mara moja.

Alisema ni matumaini yake kumuoa mama huyo wa watoto wawili na kuwa na familia naye katika siku za baadaye.

"Hatujui mpango wa Mungu ni nini lakini natamani twende kila mahali pamoja hadi mwisho," alisema.

Aidha, aliweka wazi kuwa hakuwahi kujua kuwa Hamisa Mobetto ni supastaa enzi hizo walikutana China na alikuja kujua baadaye.

Kelvin pia alithibitisha kuhusu kulipa mahari kwa mama huyo wa watoto wawili na kusema kuwa suala hilo ni kati yake na yeye.