Jalang’o akejeli ombi la Kakamega na Kisumu kuandaa AFCON, ahoji Mane atalala wapi

"Hii ni AFCON sio Chapa Dimba!” Jalang'o alibainisha.

Muhtasari

•Jalang’o alisema kuwa jiji la Nairobi lenyewe, ambalo limechaguliwa kuandaa mechi hizo haliko tayari kuandaa kwani bado kuna mengi yanahitaji kufanywa.

•Jalang'o alibainisha kuwa kando na hoteli na viwanja vya hadhi, viwanja bora vya mazoezi vinahitajika kukiwa na mashindano hayo makubwa.

Image: HISANI// FACEBOOK

Mbunge wa Lang’ata Phelix Odiwour almaarufu Jalang’o amekejeli ombi la kuandaa mechi za AFCON 2027 katika miji ya Kakamega na Kisumu.

Katika taarifa yake siku ya Jumatatu, mtangazaji huyo wa zamani wa redio alibainisha kuwa miji hiyo iko mbali sana na kuwa tayari kuandaa shindano hilo kubwa la Afrika.

Jalang’o alisema kuwa jiji la Nairobi lenyewe, ambalo limechaguliwa kuandaa mechi hizo haliko tayari kuandaa kwani bado kuna mengi yanahitaji kufanywa.

“Kabla hatujafikiria kuandaa AFCON nje ya Nairobi, tunahitaji kuandaa Nairobi! Hata Nairobi yenyewe haiko tayari! Mwaka wa 2010 nilibahatika kuandaa Kombe la Dunia nchini Afrika Kusini. Afrika Kusini ilifanya makubwa!,” Jalang’o alisema kupitia Facebook.

Aliongeza, “Tuseme tupate nafasi ya kuwa mwenyeji wa sherehe za ufunguzi, itamaanisha tutapata kuwa mwenyeji wa mataifa yote 32 yatakayoshiriki na hiyo itamaanisha kuwa tuna angalau hoteli za kifahari 32 kwa sababu nchi moja, hoteli moja. ! Ni ngapi unaweza kuhesabu kichwa? Kuandaa hafla ya ufunguzi kutamaanisha angalau wageni elfu 50 mjini, je, uwezo wa vitanda vya jiji la Nairobi ni upi? Juzi tulipokaribisha watu 5k kwa ajili ya mkutano wa hali ya hewa hoteli zote na AirBNB zote zilichukuliwa nafasi na wageni walilazimika kuhangaika kutafuta malazi, sasa unaweza kufikiria Ghana vs Nigeria iliyoandaliwa Nairobi na mashabiki wao waingie?”

Mbunge huyo wa ODM alibainisha kuwa kando na hoteli na viwanja vya hadhi, viwanja bora vya mazoezi vinahitajika kukiwa na mashindano hayo makubwa.

Aliendelea kutoa masharti magumu ya miji kama Kakamega, Kisumu na Eldoret kutimiza kabla ya kuomba kuandaa mashindano hayo ikiwa ni pamoja na kujenga hoteli kubwa na viwanja vya michezo.

“Unajua kwamba maskauti wa kimataifa wanakuja? Mahrez, Sallah, Mane na wengine wanakuja? Eldoret, Kisumu , Kakamega ngoja tutayarishe Nairobi kabla hata hujaanza ombi lenu la kuandaa AFCON isipokuwa kama hujui unachoomba kuandaa na ikiwa unayo sisitiza basi kabla ya 2027 pata angalau hoteli 10 mpya za kifahari na angalau ciwanja 2 vya viwango vya Fifa katika kaunti! Hii ni AFCON sio Chapa Dimba!” alisema.

Aidha, mwanasiasa huyo aliwaomba viongozi wa kaunti hizo kuwa na subira kwani mashindano ya AFCON ingali mbali kwani yatafanyika 2027.