Professor Hamo akiri viwango vya ucheshi wake kushuka

Muhtasari

• Hamo alikubaliana na kauli ya Andrew Kibe kwamba viwango vyake vya ucheshi vilikuwa vimeshuka.

• Alitaja janga la Corona kuwa miongoni mwa mambo yaliyosababisha hali hiyo.

Mcheshi Herman Gakobo Kago almaarufu professor Hamo amekiri kwamba viwango vyake vya ucheshi vimeshuka.

Akizungumza na mwanablogu Mungai Eve, Hamo alisema kwamba janga la Corona na kutokuwa jukwaani kwa muda mrefu vilikuwa baadhi ya vyanzo vya hali hiyo.

"...Ni ukweli sijakuwa sawa kwa sababu kuna mambo mengi ambayo yamekuwa yanaendelea ila sasa tumerudi na lazima tuchape kazi," Hamo alisema.

Hamo pia alitaja hali tete iliyokuwa baina yake na mcheshi Jemutai ilipelekea yeye kutokuwa katika hali sawa ya kiakili kuboresha ucheshi wake.

Alisema kwamba kwa sasa ashaweka mambo yote sawa, hivyo kujenga mazingira mazuri ya kurejelea na hata kuboresha kipaji chake cha ucheshi.

Kauli ya Hamo inajiri baada ya Andrew Kibe kusema katika moja ya video aliyopakia katika akaunti yake ya Youtube kwamba mcheshi huyo amepoteza ukwasi wake katika fani hiyo.

Ifahamike kwamba kipindi cha Churchill show kiliweza kurejea rasmi baada ya kuzama kwa takriban miaka miwili huku Hamo akiwa miongoni mwa wacheshi ambao walifanikiwa kupanda jukwaani wikendi jana.

Kwa sasa aliwataka mashabiki zake kuzidi kumsapoti huku akidokeza kwamba huenda pia akazamia zaidi katika tasnia ya muziki.