Mniombee kichwa kikae sawa, Harmonize awaomba mashabiki

Muhtasari

• Harmonize ameweka wazi kwamba afya yake ya akili haipo sawa na kuwataka mashabiki kumuombea.

• Alikuwa akiyazungumza haya akiendelea kusherehekea tuzo za TMA.

Staa wa muziki kutoka Tanzania, Harmonize amekiri kwamba afya yake ya akili haiko sawa na kuwataka mashabiki zake kumuombea.

Kupitia ujumbe ambao alichapisha katika ukurasa wa Instagram, Harmonize alisema anapitia kipindi kigumu huku akiamini kwamba atarudiana na mpenzi wake wa awali, Frida Kajala.

Baadhi ya mashabiki walimuonya dhidi ya kufukuzia penzi lake na Kajala wakimtaka azingatie muziki na kuboresha maisha yake.

Kondeboy alikuwa akiyasema hayo akiendelea kusherehekea tuzo za Tanzania Music Awards ambapo alifanikiwa kushinda tuzo tatu.

Alisema kwamba baada ya kuhakikisha anafufua uhusiano wake na Kajala, atakuwa anaangazia tuzo zinazokuja huku akitoa ahadi ya kuachia miziki mikali.

Aidha, mwanamuziki huyo aligusia kwamba hataki kushiriki katika tuzo za Grammy na BET, kwa kile alichokitaja kwamba anataka kuwahi tuzo za ndani kwa ndani kwanza.

Ikumbukwe kwamba Harmonize ni moja kati ya wasanii ambao walikuwa wamepigania sana kurejea kwa tuzo za Tanzania, kwani zinatoa motisha kwa wasanii kujituma katika kazi zao.