"Aq9ine akishauriwa vizuri anaweza kuwa mpishi wa kimataifa" - Pauline Njoroge

Mwanablogu huyo alisema kijana huyo anaonekana kuwa na ari nzuri ya kutaka kuwa mpishi wa vyakula mbalimbali

Muhtasari

• "Ni wazi anakosa ushauri na mwongozo kutoka kwa mtu katika sekta hiyo, ambayo ingemtia nguvu" - Pauline Njoroge

Mkuza maudhui Aq9ine na mwanablogu Pauline Njoroge
Mkuza maudhui Aq9ine na mwanablogu Pauline Njoroge
Image: Facebook, Instagram

Mwanablogu wa muungano wa Azimio la Umoja One Kenya, Pauline Njoroge amekuwa mtu wa hivi punde kuzamia mjadala unaoendelea mitandaoni kuhusu mkuza maudhui wa TikTok Aq9ine kusemekana kulazwa katika hali mbaya ya kiafya kutokana na kula buibui.

Mkuza maudhui huyo wikendi iliyopita alipakia picha kweney ukurasa wake akisema kwamba amelazimika kulazwa hospitalini katika hali mbaya kwa kupika na kula buibui.

Kwenye picha hiyo ambayo imesambazwa mitandaoni, Aq9ine anaonekana akiwa na mapeto na makunyanzi mabaya usoni yakiashirikishwa na uvimbe.

Kulingana na Pauline Njoroge, mkuza maudhui huyo ana ari sana ya kupika na kula viumbe tofauti tofauti kwa hiyo ana ndoto nzuri sana ya kuwa mpishi na anachohitaji ni kushikwa mkono tu ili kufunzwa njia salama ya kupika vyakula vyake na pindi hilo litakapofanyika basi atakuwa mpishi mmoja matata sana wa kushabikiwa kote duniani.

“Baada ya kusoma hadithi kuhusu mvulana anayeitwa Aq9ine ambaye uso wake ulikuwa umevimba baada ya kula buibui, nilipata hamu na kutembelea ukurasa wake wa Instagram. Nilitazama video zake moja baada ya nyingine na nikagundua mtu huyo ana msukumo mkubwa ya kupika na kuandaa vyakula vitamu mbalimbali. Akishauriwa na kuandaliwa ipasavyo anaweza kuwa mpishi wa kiwango cha kimataifa,” alisema Pauline Njoroge.

Aidha, mwanablogu huyo ambaye anashabikiwa sana nchini alisema kwamba tatizo la kijana huyo ni moja kwamba hajatulia na anataka kuwafurahisha mashabiki wake kwa kupika na kula viumbe mbali mbali bila kujali afya yake na hilo huenda litakuwa tatizo kwa yeyote atakayejitokeza kumshika mkono ili kumfaidi na elimu ya upishi unaofaa.

Njoroge alisema kijana kama huyo anahitaji himizo na kuongozwa vyema ili ndoto hiyo yake ya kujaribu mapishi ya vyakula kutoka Wanyama na wadudu mbalimbali wa kutisha isididimie bure bilashi.

“Shida ni kwamba yeye ni mchanga, ana msisimko wa kujaribu vitu vya hovyo, na ana enhee kidogo. Ni wazi anakosa ushauri na mwongozo kutoka kwa mtu katika sekta hiyo, ambayo ingemtia nguvu. Vinginevyo naona uwezekano mkubwa hapa ikiwa talanta yake ingeelekezwa ipasavyo,” Njoroge alisema.