Ringtone kuachia ngoma yake ya mapenzi Jumanne "Wekeni bando tayari"

Wiki mbili zilizopita, Ringtone alitangaza kugura injili na kuingia sanaa ya miziki ya kidunia.

Muhtasari

• Ringtone alisema kwamba atabadili jina lake na kujiita Bringtone pamoja na kuvalia macheni makubwa kama wasanii wa sekula.

• Alisema anagura injili kwa sababu wasichana wengine walikuwa wanamfuata badala ya kufuata Yesu.

Image: Instagrsam//RingtoneApoko

Aliyekuwa msanii na mwenyekiti wa wasanii wa injili, Ringtone Apoko ana jipya kwa wafuasi na mashabiki wake wote. Ringtone anasema baada ya kugura injili zaidi ya wiki mbili zilizopita, sasa ngoma yake ya kwanza ambayo amedokeza itakuwa ya kimapenzi itadondoka wiki kesho siku ya Jumanne.

Msanii huyo ambaye ana vituko na utata mwingi aliweka wazi kwamab kwa wale bado waanfikiria ni vitimbi anajaribu kufanya ili kufukuzia kiki mitandaoni basi waunge bando tayari kwani Jumanne ataachia ngoma ambayo itafunika zote zilizopo sokoni kwa sasa hivi.

“Ndio siku ya Jumanne, ngoma yangu ya Kwanza kama Bringtone itakuwa inadondoka. Nunueni bando na mkuwe tayari, sawa sawa,” Ringtone anaonekana akizungumza kwenye video aliyopakia Instagram yake huku akiongea kwa mtindo wa kuvuta maneno na lafudhi ya wasanii wa miziki ya kidunia.

Ringtone aliweka wazi kwamba hatimaye baada ya miaka mingi kwenye fani ya miziki ya kidunia, ameamua kugura baada ya kujipata anafuatwa na wanawake wengi ambao badala ya kumfuata Mungu wameamua kumfuata yeye.

Pia alisema lengo lake la pili kujibwaga kwenye miziki ya kidunia ni kutaka kung’oa msanii Diamond Platnumz kwenye ramani ya Sanaa ya Kenya pamoja na kuitokomeza miziki ya igeni kwenye mawimbi ya vyombo vya habari nchini, ngoma ambazo kulingana na Ringtone zimeteka anga yetu kwa sababu wasanii wa humu nchini wameshindwa kuzipoteza kwa kuachia ngoma za kidunia nzuri zenye ladha kali.

Ringtone amekuwa msanii wa injili ya kizazi kipya wa hivi karibuni kufuata umaarufu na mihela vitu ambavyo vinasemekana kuwa kwa wingi upande wa miziki ya kidunia kuliko fani ya injili.

Amewafuata watangulizi wake Bahati ambaye anawania ubunge Mathare kwac tikiti ya chama cha Jubilee na mkurugenzi mkuu wa lebo ya Saldido, Willy Paul.

Sasa kila mtu anangoja kama ni kweli Jumanne Ringtone ataachia kibao cha kidunia kama ambavyo ameahidi ama itakuwa ni uongo maana wengi wa mashabiki wake walioachia maoni walisema kwamab msanii huyo anawachezea shere kwani wanavyomjua na jinsi alivyokuwa akiwakashfu Bahati na Willy Paul basi itakuwa vigumu kuwafuata kweney miziki ya kidunia.