"Mimi ndiye msanii pekee Kenya anayepata pesa nyingi" - Bahati

Msanii huyo alisema pia ndiye msanii wa kiume pekee mweney ufuasi mkubwa mitandaoni.

Msanii na mwanasiasa bahati
Msanii na mwanasiasa bahati
Image: Instagram//Bahati

Msanii Bahati kwa mara nyingine tena ameweka wazi ni kwa nini alikataa ombi la muungano wa Azimio la Umoja One Kenya kumuahidi kazi katika serikali pindi atakapojiondoa kwenye kinyang’anyiro cha ubunge Mathare na kumuunga mkono mbunge wa sasa Anthony Oluoch.

Akizungumza katika kipindi kinachoongozwa na mchekeshaji Dr. Ofweneke, Bahati alisema kwamba si eti anaringa lakini yeye anajua tayari ako na kazi na hakuwa anataka kazi ingine bali alikuwa analenga kuwawakilisha vijana si tu wa Mathare ila kwa vijana wote nchini Kenya bungeni.

Mwanasiasa huyo aliyetamba kwa kibao cha ‘Mama’ alisema kwamba yeye ndiye msanii anayelipwa hela nyingi zaidi nchini Kenya na hiyo ni kazi tosha ambayo inamlipa.

“Kuahidiwa kazi ni kitu kizuri, lakini muda wa kunipa kazi ulipita. Mimi tayari nina kazi yangu. Sitaki kujishaua na kuringa lakini nafikiri mimi ndiye msanii wa pekee kutoka nchini Kenya anayepokea hela ndefu, kwa hiyo mtu yeyote anayetaka kunipa kazi anafaa ajue tayari mimi nilikuwa na kazi,” Bahati alitetea uamuzi wake wa kukaidi takwa la Raila.

Msanii huyo pia alitamba kwa kusema kwamba yeye ndiye msanii wa kiume nchini Kenya kuwa na ufuasi mkubwa mitandaoni, na pia kusema ndiye wa kwanza kupokezwa 'Golden Button' kutoka YouTube kwa kufikisha wafuasi milioni moja nchini Kenya, wa pili nyuma ya msanii Otile Brown.

Msanii huyo amekuwa akikumbana na visingiti si haba katika azma yake ya kuwania ubunge Mathare ambapo mara ya kwanza alishinda katika kura za mchucjo na chama cha Jubilee kikamnyima tikiti, baada ya kulia na kutokwa machozi hadharani, chama hicho kiliridhia na kumpa tikiti.

Baadae mpeperusha bendera wa muungano pana wa Azimio la Umoja One Kenya, Raila Odinga alimtaka kujiondoa kwa kile alisema msanii huyo hana uungwaji mkono sana na kumtaka kumuunga mkono mbunge wa sasa ambaye anaonekana kuwa na ufuasi mkubwa.

Bahati walitofautiana na katibu mkuu wa chama cha ODM Edwin Sifuna na mpaka kurushiana cheche za nguoni huku Sifuna akimtaka Bahati kutii matakwa ya vigogo wa muungano, kwa upande wake Bahati aligoma na kusema yuko kwenye kipute mpaka debeni.