"Hata angenitukana ningemuelewa" - Madam Rita azungumzia kumkatalia Harmonize BSS

Madam Rita adai kumkatalia Harmonize BSS kulimjenga kuwa msanii mkubwa alivyo sasa hivi.

Muhtasari

Madam Rita alikuwa miongoni mwa majaji waliomkataa Harmonize kwamba hajui kuimba wakati wa tamasha la BSS.

Madam Rita anasema kwamba Harmonize angemtukana angemuelewa.
Madam Rita anasema kwamba Harmonize angemtukana angemuelewa.
Image: Instagram

Moja kati ya matukio yanayozunumziwa sana mitandaoni ni video ya msanii Harmonize kipindi akiwa hajachipukia kabisa akiwa anajaribu bahati yake katika tamasha la kutambua vipaji la BSS nchini Tanzania.

Katika video hiyo, Harmonize alionekana akifika katika uwanja wa Mkapa Dar es Salaam kupanga mlolongo kati ya maelfu ya vijana waliokuwa wanajaribu kuonesha vipaji vyao ili kushikwa mkono.

Harmonize alipopanda jukwaani ambapo majaji walikuwa ni Master J, Madam Rita miongoni mwa wengine walimkataa na kumwambia kwamba hana kipaji cha kuimba na pengine ajaribu kufanya kitu kingine lakini si muziki.

Miaka mitano baadae, Diamond alimshika Harmonize mkono na kumtoa kimuziki ambapo mpaka sasa amekuwa mwanamuziki wa kutajwa na wengi.

Kinachoshangaza wengi ni jinsi ambavyo Harmonize amekuwa akilipa fadhila zake kwa majaji hao haswa, Rita ambaye amekuwa akimsifia mara nyingi tu hata kwenye wimbo wake akisema yeye ndiye alimfanya kutia bidi kabisa baada ya kumuambia kwamba hajafika viwango vya kuwa msanii.

Kipindi kimoja pia Harmonize aliwahi kumuita Rita jukwaani akitumbuiza na kumsujudia kwa magoti kwa kumshukuru kwamba kule kumkatalia kulimtia hamasa ya kujibidiisha kimuziki.

Hatimaye madam Rita amelizungumzia tukio hilo zima na kumtaja Harmonize kuwa kitu kinachomfanya kuendelea kukwea ni unyenyekevu wake. Pia Rita alisema kwamba Harmonize hata angemtukana angemuelewa kutokana na kile walimfanyia wakati wa majaribio ya BSS.

“Hata angepanda jukwaani na akanisema kwa kunitusi kwenye nyimbo yake mimi  ningemuelewa kwa sababu labda anaeza akawa na hasira pale BSS alipita tukamkatalia lakini miaka 5 baadae akafanya kinyume na jinsi tulivyotarajia,” Madam Rita alizungumza.

Ila pia madam Rita ambaye anajulikana kuwa mshika dau mkubwa sana katika kukuza vipaji vya muziki Tanzania alisema kwamba kitendo cha wao kumkatalia katika BSS kulimjenga sana na kumfanya mtu ambaye amekua sasa hivi.