Mchungaji wa kike aliyebuni maneno ya "Twa Twa" kuchukua hakimiliki ya maneno hayo

Video ya mchungaji Sue Munene akitumia maneno ya "twa twa" kurejelea kitendo cha kushiriki mapenzi na mumewe ilisambaa 2019.

Muhtasari

• Mchungaji huyo alisema hatua yake ya kuchukua hakimiliki si kuwafungia watu wasitumie maneno hayo bali ni kuwa na umilisi kama muasisi wake.

• Notisi hiyo ya mamlaka ya kutoa hakimiliki ilimtaka mtu yeyote anayepinga ombi la Munene kuwasilisha malalamiko kwa siku 60.

Mchungaji Joseph na Sue Munene, waanzilishi wa maneno ya "Twa Twa"
Mchungaji Joseph na Sue Munene, waanzilishi wa maneno ya "Twa Twa"
Image: Instagram

Mchungaji Sue Munene, aliyepata umaarufu wa ghafla mwaka 2019 kufuatia maneno yake ya ‘twa twa’ akirejelea kitendo cha kushiriki mapenzi na mumewe, sasa ameibuka akisema kwamba anataka kuchukua hakimiliki za maneno hayo.

Maneno ya “twa twa” yamekuwa yakitumiwa na makundi ya watu wengi katika sajili mbalimbali aghalabu wakati wa kuzungumzia suala la tendo la ndoa.

Katika mahojiano ya kipekee na Sunday Nation, Sue Munene alisema kuwa hatua yake ya kuchukua hakimiliki za maneno hayo si kuwafungia watu kutoyatumia bali ni kupata tu utambuzi kama muasisi wa maneno yenyewe.

“"Ni umiliki, sio kwa madhumuni mengine yoyote. Sio kwa biashara, sio kwa chochote. Unaona jinsi watu wanavyosema wanataka kulipwa? Huo ni ubinafsi,” Munene aliambia jarida hilo.

Maneno ya mchungaji huyo yamekuwa yakitumiwa pamoja na sauti yake na wasanii wengi wa humu nchini, na awali aliyatamka akitolea mfano kwamba ndoa yoyote haifai kukosa kushiriki mapenzi, kitu alichokiita “twa twa” kama njia moja ya kukwepa kutumia lugha wazi na tambarare isiyo na stara.

 Alisema kwamba yeye hushiriki tendo la ndoa (twa twa) na mumewe kila muda, sehemu yoyote hata wakati ule wamekosana, kwani kitendo hicho ndicho msuluhishi mkuu na hodari katika ndoa yoyote.

Alama inayopendekezwa ni tagi ya sauti isiyo ya kiisimu inayojulikana na (mwombaji) inayoashiria ukaribu wa uhusiano,” mamlaka ya kutoa hakimiliki ilifichua ikirejelea ombi la Munene kutaka kupewa haki hizo.

Mchungaji Sue alisema yeye na mume wake, wanaohudumu katika Kanisa la Overcomers Hope Ministry Nairobi, kanisa waliloanzisha, walikuwa wakifikiria kupata chapa hiyo tangu miaka mitatu iliyopita.