Msanii mkongwe wa kizazi kipya kutoka Tanzania, Marlaw kwa mara ya kwanza baada ya kwenda kimya kwa Zaidi ya miaka kumi, amezungumza sababu za kuingia gizani muda huo wote na mipango yake ya kurejea tena kwenye muziki.
Akizungumza na runinga ya East Afrika, Marlaw alisema kuwa hakuondoka kwa muziki kwa njiay a shari bali aliwapisha makinda kidogo ili naye akapate kuwatazama jinsi wanaendesha Sanaa ya muziki.
“Nilipokuwa ilikuwa ni katika kupumzika naeza nikasema. Au kujiandaa hivi kwa sababu unajua nilikuwa nimejihisi nimefanya sana na hadi ikafika muda nikaona kwamba na mimi sasa naweza nikatulia kidogo ili nifanye tena baadae kama itawezekana,” Msanii huyo alisema.
Marlaw alisema baada ya kuangalia kwa mbali aligundua kuwa watu wengi walikuwa wanamtazamia yeye na hivyo kumpa msukumo wa kurudi tena kwenye muziki.
“Nimeandaa vitu vingi sana, unajua muda nilioupata nadhani nimeandaa baadhi ya vitu vizuri, naziita kama zawadi kwa mashabiki wangu. Nimekaa nje tangu mwaka 2010 hadi sasa,” Marlaw alisema.
Katika kipindi chote, Marlaw alisema kuwa amekuwa akifanya biashara yake ya mauzo kujiendeleza ila akasema kwamba hakuwa anapata kipato kizuri kama kile ambacho alikuwa akikipata kutoka kwa muziki.
“Zaidi mtu unaishi kwa kushikwa mikono sababu unazungukwa na watu, familia jamaa na marafiki,. Kwa hiyo huwezi ukasema unaweza mwenyewe. Lakini mimi nimepata sapoti kubwa sana mpaka kufikia hapa nahisi niko tayari kurudi,” alisema.
Msanii huyo alisema kuwa furaha kubwa anayopata maishani mwake ni kupatana na watu waliokuwa mashabiki wa ngoma zake nyingi na kumwambia kwamba kupitia kwa nyimbo zake ndio walipatana na kupendana na sasa hivi wametulia wanalea familia.