Namuombea Wema Sepetu aweze kupata familia, mtoto - Mamake Kanumba

“Yule mtoto Wema, namuombea kwa Mungu. Hajawahi nitukana, hajawahi nikashifu, hajawahi nisema vibaya na sitarajii kama hilo litakuja kutokea" - Mama Kanumba.

Muhtasari

• “Kwenye mahusiano mapya naomba Mungu asimame kati. Wamtangulize mungu, mimi hiyo couple yao naifurahia, naiunga mkono lakini wamtangulize Mungu,” alisema.

Mama Kanumba afichua ukaribu wake na Wema Sepetu.
Mama Kanumba afichua ukaribu wake na Wema Sepetu.
Image: Screengrab, Instagram

Mama Kanumba amepuuzilia mbali dhana kwamba mwigizaji Wema Sepetu hapati mtoto kutokana na laana aliyotamkiwa na Kanumba kwa kuavya mimba zake.

Katika mahojiano na Global TV Online, Bi Mutegoa alisema kuwa katika watu wengi ambao Kanumba aliwainua na kuwatambulisha kwenye Sanaa ya uigizaji, Wema Sepetu ndiye mmoja wao ambaye hajawahi kumtukana wala kumuonyesha madharau.

Alisema kuwa yeye na Wema ni marafiki wakubwa na kila siku anamuombea kwa Mungu kumpa familia lakini pia mtoto – kitu ambacho Wema amekuwa akikihitaji kwa muda mrefu sasa.

“Yule mtoto Wema, namuombea kwa Mungu. Hajawahi nitukana, hajawahi nikashifu, hajawahi nisema vibaya na sitarajii kama hilo litakuja kutokea. Nikimpigia simu anasema mama shikamoo, unaendelea aje. Yaani yule mtoto namuombea kwa Mungu ampe maisha marefu aweze kupata familia mtoto basi tu. Hajawahi nichoka,” alisema Bi Mutegoa.

Pia aliweza kuzungumzia uhusiano wa mrembo huyo na msanii Whozu na kusema kuwa anaona wako sawa na wanachofaa kukizidisha Zaidi ni maombi yao kwa Mungu.

“Kwenye mahusiano mapya naomba Mungu asimame kati. Wamtangulize mungu, mimi hiyo couple yao naifurahia, naiunga mkono lakini wamtangulize Mungu,” alisema.

Bila shaka wengi wanafahamu na hata Wema mwenywe si mara moja au mbili amewahi simama mbele ya vipaza sauti akikiri kwamba maisha yake ya sasa hivi hayangekuwa hivi pasi na mchango wa marehemu Kanumba.

Sepetu alisema kuwa Kanumba alimpata baada ya kushinda Miss Tanzania mwaka 2006 na akampa jukumu la kuigiza kwenye filamu, kitu ambacho leo hii ukimuuliza ni nini anakifurahia Zaidi kati ya uanamitindo na uigizaji basi muda wote atakutajia uigizaji.

“Nisiseme uongo mimi nafurahia sana nikiwa mbele ya kamera naigiza. Nafurahia sana kwa sababu yaani naipenda sana ile kazi ya kuigiza. Mimi nimeanzia katika tasnia ya urembo lakini nimeonekana Zaidi nilivyoingia kwenye tasnia ya filamu. Kuwa Miss Tanzania kilikuwa kitu kimoja lakini pia kuwa mwigizaji kulikuwa kitu kingine kikubwa na tofauti kabisa,” Sepetu aliiambia Manara TV katika mahojiano ya awali.