EXCLUSIVE

Kutoka kumiliki baa ya 17m hadi kuwa fukara - mkongwe wa Ohangla Atommy Sifa

"Wezi walikuja wakaiba runinga zote, wakaiba mtaji pamoja na ala zangu zote za muziki. Wakanirudisha chini sana mpaka sasa nimeshindwa kuamka," Atommy Sifa alisema kwa hisia.

Muhtasari

• Atommy Sifa alisema kwamba hangekuwa anaomba msaada wa kifedha kama si wezi kuvunja moja ya klabu yake ya starehe katika kaunti ya Homa Bay mwaka jana.

• Msanii huyo alisema kwamba alikuwa amewekeza mtaji wa shilingi milioni 17 pesa za Kenya katika biashara ya baa.

Atommy Sifa.
Atommy Sifa.
Image: Facebook

Mkongwe wa muziki wa Ohangla Atommy Sifa amefunguka jinsi amejipata katika hali ngumu ya kulazimika kuitisha msaada wa kifedha mitandaoni licha ya kuwa mmoja kati ya wasanii waliokuwa wanavuna pakubwa kutokana na muziki huo pendwa na jamii zinazozingira ziwa Victoria.

Katika mahijiano ya kipekee kwa njia ya simu na mwandishi wa Radio Jambo, Atommy Sifa alikiri kwamba katika maisha yake hakuwahi kufikiria kwamba angekwenda wazi mitandaoni na kuwalilia watu kumkwamua kifedha.

Lakini amelazimika kufanya hivyo baada ya mambo yake kugonga mwamba, hali ambayo anaisingizia kwa tukio la wizi lililotokea katika biashara yake kubwa ambayo alikuwa amewekeza karibia mtaji wake wote.

Atommy Sifa alisema kwamba hangekuwa anaomba msaada wa kifedha kama si wezi kuvunja moja ya klabu yake ya starehe katika kaunti ya Homa Bay mwaka jana.

Msanii huyo alisema kwamba alikuwa amewekeza mtaji wa shilingi milioni 17 pesa za Kenya katika biashara ya baa lakini kwa bahati mbaya wezi walivunja baa hiyo na kuiba bidhaa ikiwemo vyombo vya sanaaa, jambo lililompiga dafrau ka kumrudisha katika hatua ya sifuri.

“Nilikuwa na baa Rockcity Jungle Resort, sasa wezi walikuja wakaiba runinga zote, wakaiba mtaji pamoja na ala zangu zote za muziki. Wakanirudisha chini sana mpaka sasa nimeshindwa kuamka. Tangu hapo baa yangu ilifunga milango kwa sababu walibeba mtaji wote wa 800k na kila kitu. Klabu nilijenga na shilingi milioni 17,” Atommy Sifa alisema.

“Pesa zangu zote ziliisha kwa sababu niliwekeza mtaji wangu wote pale na zingine nikanunua ala. Ni kama utumie pesa kujenga kitu halafu kibaki kama kimechomeka. Sikuwa nimechukua bima yoyote kwa sababu ndio nilikuwa nimefungua. Wakati ule niko katika harakati ya kupata bima na leseni, ikabebwa yote,” msanii huyo alisema.

Atommy Sifa alisema yeyote ambaye ana moyo wa kutaka kumsaidia ili kumuinua kutoka mavumbini tena anaweza fanya hivyo kupitia kwa namba yake ya simu 0725763370, akisema tangu wikendi hadithi hiyo yake ya kutia huruma ilipovuja, wengi wamempigia simu kumpa ahadi na baadhi kumpa mchango mpaka sasa shilingi elfu 18.