"Mimi sio iluminati" Mwanawe waziri wa zamani Mutahi Kagwe, Kahush asema

Kahush alinyoosha maelezo kuhusu pete yenye jicho moja katika kidole chake ambayo ishara yake inahusishwa na jumuiya yenye itikadi ya iluminati.

Muhtasari

• "Hii ni pete tu ya kawaida na haina uhusiano wowote na iluminati. Mimi siko katika iluminati.”

Kahush
Kahush
Image: Instagram,

Msanii wa muziki wa Rap, Kahush ambaye pia ni mtoto wa waziri wa zamani wa afya Mutahi Kagwe amefunguka kuhusu ujumbe fiche ambao alipakia kwenye ukurasa wake wa Instagram siku chache zilizopita.

 Kwenye Instagram yake, Kahush alipakia ujumbe unaosema kwamba ameshauza nafsi yake, jambo ambalo liliwafanya wengi kuelewa kwa njia tofauti tofauti wengine wakisema kwamba amejiunga na kundi la itikadi hasi la iluminati.

“Kauli hiyo ni changamano kidogo kuliko vile wengi wanaona lakini nitalizungumzia hilo muda mwingine huko mbele,” Kahush alisema akicheka.

Kuhusu pete ambacho alikuwa amevalia kwenye kidole chake cha kati, pete ambayo ina ishara ya jicho moja ambayo inahusishwa pakubwa na kundi la iluminati, Kahush alinyoosha maelezo akisema;

“Hapana, hii pete kwangu ina maana kwamba ‘weka jicho lako wazi, weka jicho lako kwenye zawadi’ na huwa naivalia katika kidole changu kwa sababu unajua wakati ninashambulia maisha itakuwa ni kama ninatazamia kukipata kila kitu. Hii ni pete tu ya kawaida na haina uhusiano wowote na iluminati. Mimi siko katika iluminati.”

Kahush juzi kati alikuwa mmoja wa wasanii waliotumbuiza katika tamasha lililoandaliwa kuadhimisha miaka 50 ya muziki wa HipHop weney chimbuko lake Marekani na ambao katika muda umesambaa kwenye mataifa karibia yote duniani.

“HipHop kufikisha miaka 50, unajua mtu kama mimi nimekua tu muda wote nikisikiliza HipHop kwa hiyo nimekuwa nikiujua muziki huu kama wa tangu enzi za kale sana. Hata nilipoambiwa kwamba ndio mwanzo unaadhimisha miaka 50 nilishangaa mbona 50 miaka kidogo sana lakini muda wote nausikiliza muziki huo na miziki mingine ambayo imetokana na HipHop kwa sababu hata muziki ambao ninaufanya umetokana na HipHop,” alisema.

Kama tu Khaligraph aliyemsifia pakubwa Nyashinski, Kahush naye alisema kwamba anapenda sana kumfuatilia msanii huyo mkongwe kwa njia kubwa sana.

“Napenda kusikiliza ngoma za Nyashinski, kwangu mimi huyo ndiye msanii wangu pendwa sana, pia nasikiliza Octopizzo na hao ndio wasanii wangu nawatambua. Khaligraph namsikiliza tu lakini si vile kama ninavyowasikiliza wengine,” alisema.