Nandy amuongeza yaya mshahara mara 2, amuahidi iPhone 15 kwa kulea mwanawe vizuri

Nandy alitangaza kumuongeza dada wa kazi za nyumbani mshahara na mumewe Billnass akasema simu za iPhone 15 zitakapowasili madukani mwezi Septemba, ya kwanza itakuwa ya yaya huyo.

Muhtasari

• Za chini ya zulia zinakisia kwamba Bei ya iPhone 15 nchini Kenya itakuwa Ksh. 260,000. Bei pia itategemea Bei ya iPhone 14 mpya na iPhone 14 Pro.

• Wengi wamesema yaya huyo anastahili kwani amekuwa na mtoto muda wote Nandy akiwa kwenye shughuli za usanii mpaka wengi kuhisi hana mtoto.

Nandy ampa mjakazi Iphone
Nandy ampa mjakazi Iphone
Image: Instagram

Famialia ya msanii Nandy na mumewe Billnass wamemfanyia kitendo cha heri mjakazi wao wa nyumbani kwa kazi nzuri ambayo ameifanya kulea mwanao ambaye hivi majuzi amefikisha mwaka mmoja.

Kwa mujibu wa taarifa ya kipekee kwenye chaneli ya Ayo TV, Nandy alipokuwa ameandaa tafrija la watoto kumsherehekea mwenzao kutimiza mwaka mmoja, alimwita mamake na yaya wake mbele na kutoa tamko kwamba atamuongeza mshahara wake kwa mara mbili Zaidi kama njia moja ya kurudisha mkono wa fadhila na shukrani.

Taarifa hiyo ilizidi kueleza kwamba kwa upande wake mumewe Nandy, Billnass, naye alijitolea kumpa yaya wao simu ya kifahari ya iPhone.

Billnass alimtaka dada huyo wa kazi za nyumbani kuchagua ni iPhone gani anataka kati ya iPhone 14 ambayo iko masokoni kwa sasa au ile ya iPhone 15 ambayo itatua masokoni mwezi Septemba.

Yaya alichagua kuvuta subira na kuingoja ile ya iPhone 15 na Billnass – ambaye ni mjasiriamali wa bidhaa za kielektroniki kama simu na kompyuta akasema pindi simu hizo zitakapowasili kwenye duka lake, simu ya kwanza ya iPhone 15 itakuwa ni mjakazi wake.

"Nimetoa shukrani ya kipekee kwa dada wangu wa nyumbani, amekuwa kama familia kwa sababu sasa hivi ana mwaka wa tatu kwangu, nimekuwa naye tangia bado sina unauzito. Ameshika hadi tarehe za kliniki. Tumemzawadia kumuongezea mshahara mara mbili nimemuambia, mwezi ujao tutampa iPhone 15. Tunampenda sana na hongera kwa wazazi waliomlea." Nandy alisema.

IPhone 15 inatarajiwa kuzinduliwa mnamo Septemba 12, ambayo kampuni bado haijathibitisha rasmi. Lakini, Apple inatarajiwa kutangaza tarehe ya tukio lake kubwa lijalo katika siku zijazo. Bei, vipimo, muundo na kila kitu tayari vimevuja mtandaoni kabla ya uzinduzi, unaotarajiwa kuwa baada ya wiki chache. Hapa kuna maelezo.

Za chini ya zulia zinakisia kwamba Bei ya iPhone 15 nchini Kenya itakuwa Ksh. 260,000. Bei pia itategemea Bei ya iPhone 14 mpya na iPhone 14 Pro.

 Uvumi ulidai kuwa iPhone 15 ya mwaka ujao itakuwa na onyesho la OLED na kihisi cha Kitambulisho cha Uso ambacho kitawekwa ndani ya skrini.

Mwanawe Nandy, Kenaya alifikisha umri wa mwaka mmoja Jumatatu wiki hii na ndio ilikuwa mara ya kwanza kwa msanii huyo kupakia picha hadharani na pia kulitaja jina la binti yake ambaye amemficha kwa miezi 12 iliyopita hadi kuwafanya baadhi kuhisi kwamba hana mtoto.

Muda wote huo akifanya shughuli zake kama kawaida, yaya ndiye alikuwa mlezi wa mwanawe na hivyo kuona anastahili zawadi hiyo ghali lakini pia kuongezewa mshahara.