Nilijengea wazazi wangu nyumba nikiwa na umri wa miaka 13 tu! - Aslay

"Nimekuja kupata mafanikio makubwa wakati tayari mama keshafariki, lakini mamangu alikuwa ni mtu ambaye alipenda kumuona mwanawe anafika sehemu Fulani,” Aslay alisema machozi yakimlengalenga machoni.

Muhtasari

• Mamangu alikuwa ni mtu mzuri na ambaye alipenda kuona mafanikio yangu japo kuwa mpaka anaondoka sidhani kwamba alikuwa amefaidi sana kutokana na jasho langu - Aslay.

Aslay.
Aslay.
Image: Screengrab.

Msanii Aslay amefichua kwamba aliwajengea nyumba wazazi wake kabla ya kifo cha mamake akiwa na umri wa miaka 13 tu.

Msanii huyo ambaye alijijengea jina kwenye Bongo Fleva na kupata mafanikio na umaarufu akiwa mdogo alifichua hata katika mahojiano na Ayo TV wakati anaendelea kupigia debe na upato tamasha lake la mwisho wa Septemba kusherehekea na kuadhimisha miaka 10 kwenye muziki huo uliomkuza na kumlea.

Aslay ambaye mara nyingi amekuwa akizungumzia kwa uchungu jinsi kifo cha mamake kilimkwaza na kumtoa kwenye reli ya muziki kwa muda alisema kwamba kwa sasa nyumba hiyo anaishi babake na mwakamke mwingine ambaye alikuja kuoa baada ya mamake Asay kufa.

“Nilijenga nyumba na kuimalizia kila kitu freshi na sasa hivi anakaa babangu na… kwa sababu baba sasa hivi kaoa ana mwanamke mwingine, ana mdogo wangu pia amejifungua mamangu wa kufikia. Niliweza kuwajengea wazazi nyumba nikiwa na miaka 13 wakati huo. Nilijenga nyumba moja kwa sababu walikuwa wanaishi pamoja mama na baba,” alisema.

Aslay alisema kwamba ushawishi wa mamake kipindi hicho ulichangia pakubwa maamuzi ya kumjengea kwanza kinyume na ndoto za vijana wengi kupata umaarufu jambo la kwanza ni kujifikiria weneywe kupata magari mazuri ya kifahari, lakini yeye alishawishiwa na mama kukumbuka nyumbani kwanza.

“Hiyo nguvu ya kusema ningenunua gari langu au kununua nyumba yangu kwanza kipindi kile nilikuwepo sina kwa sababu mamangu alikuwa anani-control kwa kila kitu. Yaani kwamba hata nikimdanganya nimefanya shoo nimepata sijui 200k ananiambia tuma 180k kwanza halafu hiyo 20k kaa nayo kwa sababu kwa kipindi kile alikuwa anajua huyu mtoto hana matumizi makubwa na hawezi kufanya chochote,” alisimulia.

Aslay alisema kwamba ushawishi huo wa mamake ulihakikisha kwamba amewekeza katika miradi isiyohamishika tena ya kudumu kwani bila yeye labda angezimalia hela kwa mambo ya kupita tu.

“Naweza nikasema nimejenga mimi lakini kwa nguvu kubwa ya mamangu Mariam. Unajua mama ni mama tu, mama siku zote hawezi kuwa mbaya kwa tafsiri yoyote unayoweza kuifikiria. Mamangu alikuwa ni mtu mzuri na ambaye alipenda kuona mafanikio yangu japo kuwa mpaka anaondoka sidhani kwamba alikuwa amefaidi sana kutokana na jasho langu. Nimekuja kupata mafanikio makubwa wakati tayari mama keshafariki, lakini mamangu alikuwa ni mtu ambaye alipenda kumuona mwanawe anafika sehemu Fulani,” Aslay alisema machozi yakimlengalenga machoni.