Aslay aeleza jinsi Rayvanny alivyochochea kusambaratika kwa Yamoto Band

"Rayvanny alitambulishwa WCB Wasafi na akapewa RAV4 na sisi tamaa zikatuingia tukaona kumbe hata mimi naweza toka kivyangu na nifaulu," Aslay alisema.

Muhtasari

• "Kwa hiyo Rayvanny alipotoka kila mtu akawa anatamani duh, kumbe hata mimi naweza nikafanya kitu kama hiki na nikapata mimi kama mimi" - Aslay.

Yamoto Band
Yamoto Band
Image: Insta

Msanii Aslay amekuja na dhana mpya ya kuelezea kile anahisi kilisababisha kundi lao la Yamoto Band kusambaratika miaka michache baada ya kufana chini ya uongozi wa meneja Mkubwa Fela.

Kupitia Amplifaya ya Clouds FM ikiongozwa na Millard Ayo, Aslay aliibua madai kwamba Yamoto ilifikia wakati wakaingiwa na tamaa iliyosababisha bendi ikaanza kuregarega.

Alisema kwamba kwa asilimia Fulani utambulisho wa msanii Rayvanny kwenye lebo ya WCB Wasafi uliwachochea Zaidi kila mtu kujitegemea kivyake na hivyo kuzua nyufa Zaidi kwenye Yamoto Band.

Aslay alikumbuka kwamba kipindi Rayvanny anatambulishwa na Wasafi, wao walikuwa katika ziara ya muziki Ulaya na walipomuona anatambulishwa na kukabidhiwa gari la kifahari, kila mmoja anahisi ni wakati wao pia kujiachia kivyao kwani kile walichokuwa wanakipata kama kundi kilianza kuwa haba.

“Nakumbuka wakati Rayvanny anatoka, sisi tulikuwa tuko Europe Tour, huko Ulaya. Rayvanny akapewa RAV4 kipindi kile nakumbuka. Sasa si unajua pia ndio sisi Yamoto tunaiona kabisa ndio inaregarega halafu hatuelewi. Na pia tulikuwa tushaanza kila mtu kurekodi ngoma yake moja moja. Kwa hiyo Rayvanny alipotoka kila mtu akawa anatamani duh, kumbe hata mimi naweza nikafanya kitu kama hiki na nikapata mimi kama mimi. Ujajua unapopata 10k halafu mnaigawanya na huku unaona kumbe naweza nikaiminya peke yangu. Pale ndio tamaa zilianza kuja,” Aslay alieleza.

Alisema kwamba alianza yeye kujitoa kwenye kundi baadae kila mwingine akawa pia anachukua njia yake.

Msanii huyo alikiri kwamba bosi wao Mkubwa Fela aliona hilo na kujaribu kuwaunganisha pamoja kuendeleza kundi la Yamoto lakini tayari mtumbwi ulikuwa ndio umeshazidiwa na maji.

“Alijaribu kufanya vitu kama hivyo lakini akafika muda akaona hawa watu wazima na wameshafika mahali ya kuona ni vitu vipi wanavitamani,” alisema.