Zuchu alia kuibiwa begi la mavazi aliyopanga kuvaa akitumbuiza jukwaani Rwanda

"Mimi sijawahi ku’manage msanii wa kike kwa kweli, nimeshuhudia kitu kipya, Analia mbele yangu,” alisema Babu Tale.

Muhtasari

• “Hivi ninavyokwambia natoka madukani, kusema kweli Tanzania tuna nguo na tuna machaka, hapa tumezunguka masaa 3 ndio tunarudi" Babu Tale.

Zuchu
Zuchu
Image: Instagram

Meneja wa wasanii wengi wa WCB Wasafi, ambaye pia ni mbunge Babu Tale amefichua kwamba Zuchu alipatwa na majanga makubwa akiwa safarini kwenda Rwanda alikotarajiwa kutumbuiza katika uzinduzi wa tuzo za Trace.

Babu Tale alifichua kwamba wasanii Diamond na Zuchu pamoja na yeye walitumiwa ndege ya kibinafsi kuwachukua kutoka Tanzania kwenda Rwanda lakini walipofika, Zuchu aligundua begi lake halipo na akanza kutiririkwa na machozi.

Tale alikiri kuwa hicho kilikuwa kipindi kigumu sana kwake kwani hajawahi msimamia msanii wa kike na ilimbidi yeye kuongozana naye kwenda mitaani kutafuta maduka ya kuuza nguo.

Mchakato wa kutafuta nguo za kumpendeza ili kutumbuiza uliwachukua Zaidi ya saa 2, Babu Tale akisema hata hivyo hawakufanikiwa kupata nguo nzuri kihivyo lakini akasema kwamba wote waliomba tu zimpendeze Zuchu maana hakuwa na jinsi tena begi lake lishapotea.

“Ilikuwa tuje mchana lakini tukaletewa private jet ambayo ilifika Tanzania saa tatu usiku na tuliondoka majira ya saa tano na tumefika hapa saa nane. Katika zile harakati begi la Zuchu likabakia, sijui limebakia wapi, mimi sijawahi ku’manage msanii wa kike kwa kweli, nimeshuhudia kitu kipya, Analia mbele yangu,” alisema Babu Tale.

“Hivi ninavyokwambia natoka madukani, kusema kweli Tanzania tuna nguo na tuna machaka, hapa tumezunguka masaa 3 ndio tunarudi, lakini tuombe Mungu kama atapendeza,” aliongeza.

Katika tuzo za Trace ambazo zilifanyika kwa mara ya kwanza nchini Rwanda, Kigali, Diamond na Zuchu walikuwa wameteuliwa katika vitengo mbali mbali japo Diamond pekee ndiye alishinda kama msanii bora wa Afrika Mashariki.