Brian Mwenda, jamaa aliyetajwa kama wakili na mwanasheria bandia amefichua kwamba yeye ni mshauri wa masuala ya kisheria katika mataifa mbali mbali ndani na nje ya Afrika.
Akizungumza katika stesheni ya Radio Jambo kwa njia ya kipekee na mtangazaji Massawe Japanni, Mwenda alisema kwamba ngonjera ambazo zinaenezwa mitandaoni kwamba yeye ni mwanasheria bandia si za kweli.
Mwenda hata hivyo hakutaka kuzungumzia kwa undani kuhusu kashfa ambayo imemleta kwenye mwanga wa vyombo vya habari hivi karibuni kwa kigezo kwamba ni suala ambalo bado liko mahakamani hivyo kulijadili ni sawa na kuingilia mahakama.
Mwenda alisisitiza kwamba yeye ni mshauri wa kisheria na hata kwenda mbele kufichua kwamba ana makampuni kadhaa ya kutoa ushauri wa kisheria kuhusu masuala ya watu kuibiwa pesa katika mataifa 6.
“Mimi ni mshauri wa kisheria na tayari nina makampuni ya ushauri wa kisheria katika jiji la Dar es Salaam nchini Tanzania, Accra nchini Ghana, Lagos nchini Nigeria, Birmingham nchini Uingereza na New York nchini Marekani,” Mwenda alisema.
Katika kesi ambayo inaendelea kumuandama mahakamani, Mwenda aliitaja kama ni kuwindwa kinyume cha sheria lakini akasema kwamba utafika muda watu watamuelewa na kila kitu kitakuwa sawa.
Alisema tayari ana wanasheria wanaoshughulikia kesi yake wapatao 9, akiwemo wakili bingwa Khaminwa, Omari miongoni mwa wengine.