Mwijaku ahusisha masaibu ya Whozu na mikosi ya kushiriki Wasafi Festival ya Diamond

Kwa mujibu wa Mwijaku, Diamond ni mtu mwenye mikosi na mtu yeyote anayevuta kwenye jambo lake moja kwa moja huchukua mgao wa mikosi hiyo.

Muhtasari

• Mwijaku sasa amekuja na dhana tofauti akisema kwamba masaibu yake yametokana na kukubali kushiriki katika msururu wa shoo za Wasafi Festival

Mwijaku na Whozu
Mwijaku na Whozu
Image: Instagram

Siku moja baada ya baraza la Sanaa Tanzania, BASATA kutoa tamko la kuwafungia wasanii Whozu, Mbosso na Billnass kwa muda wa kati ya miezi 3 hadi 6 na faini ya milioni 3 kwa kuachia video yenye maidhui ya kwenda kinyume na maadili na kanuni za baraza, dhana mbalimbali zimevutwa.

Whozu, ambaye ndiye mwenye wimbo na aliwashirikisha Billnass na Mbosso kwenye remix ya ‘Ameyatimba’ ndiye mwathirika mkubwa katika kichapo hicho cha BASATA.

Whozu alipigwa marufuku ya kutojihusisha kivyovyote vile na kazi ya Sanaa kwa muda wa miezi 6 na kutoa faini ya milioni 3 pesa za kitanzania.

Mwijaku sasa amekuja na dhana tofauti akisema kwamba masaibu yake yametokana na kukubali kushiriki katika msururu wa shoo za Wasafi Festival.

Kwa mujibu wa Mwijaku, Diamond ni mtu mwenye mikosi na mtu yeyote anayevuta kwenye jambo lake moja kwa moja huchukua mgao wa mikosi hiyo.

Pia mtangazaji huyo mwatukaji alikwenda mbele kumpiga vijembe Whozu kwamb masaibu yake yameendelea kwa mfululizo, ikiwa ni hivi juzi tu mamake Wema Sepetu – mpenzi wake alivamia tafrija yao na kuweka wazi kwamba hamtambui kwa vile Wema hakuwahi kumtambulisha nyumbani.

“Kweli ng'ombe wa masikini hazai . Mama mkwe hakutaki huku basata unatakiwa ulipe Milioni 6 . Alafu wakati huo huo ulipe kodi ili usidhalilike . Na show hakuna ndani ya miezi 6 . Nilikwambia kumkumbatia MWAMBINO [Diamond Platnumz] ni mkosi sasa umeamini maneno yangu,” Mwijaku aliandika akiweka picha yake na Whozu Twitter.

Ikitangaza adhabu hiyo, BASATA ilisema kwamba hii si mara ya kwanza kwao kumpa onyo Whozu mara mbili lakini wakasikitika kwamba msanii huyo hakuwahi kuzingatia onyo hizo na hivyo kuvutia adhabu hiyo kali.