Eric Omondi atoa sababu za kutofanya michango ya karo, harusi na mahari

Mcheshi huyo alisisitiza kuwa yeye huguswa tu na visa vyenye hisia nizito vinavyogusa Wakenya.

Muhtasari

• Eric Omondi  atoa sababu ni kwa nini huwa hafanyi michango ya shule,harusi nay a kulipia mahari.

• "Ninachangia watu ambao wanategemea pesa hizo kwa maswala mazito."

Eric Omondi
Eric Omondi
Image: Facebook

Mcheshi na mwanaharakati Eric Omondi ameeleza wazi sababu za kutofanya michango ya karo za shule,hafla za harusi na kulipa mahari.

Omondi amechangisha pesa kwa watu wengi wanaohitaji matibabu na mahitaji ya kifedha yanayohusiana na hali ngumu za maisha. 

Mcheshi huyo aliyegeuka kuwa mhisani, kwa kawaida huwaongoza Wakenya kupitia mitandao yake ya kijamii ili kuwasaidia wanaohitaji misaada ya dharura.

Amekuwa akionyesha kikamilifu visa muhimu vya Wakenya wanaotafuta usaidizi, haswa katika maswala ya matibabu.

Akizungumza wakati wa mahojiano ya hivi majuzi, Omondi alieleza kuwa hawezi kusaidia watu ambao wamekuwa wakitafuta usaidizi nje ya masuala ya matibabu kwa sababu atashawishika kuchukua sehemu ya pesa zilizochangishwa.

Mcheshi huyo alisisitiza kuwa yeye huguswa tu na visa vyenye hisia nzito vinavyogusa Wakenya.

"Hatuchangii pesa za karo za shule au harusi au vitu kama ruracios (sherehe za kitamaduni). Mambo kama hayo naweza kujaribiwa kuchukua pesa na kujihifadhi. Ninachangia watu ambao wanategemea pesa hizo kwa maswala mazito. Ukigusa hizo pesa, unaweza kulaaniwa. Tunashughulika na upandikizaji wa figo, mtu ambaye mwanawe amekuwa katika chumba cha kuhifadhia maiti kwa miaka mitano na kwa hivyo singewahi kufanya hivyo. Singeweza kamwe kuchukua kiasi chochote kutoka kwa maswala kama haya,” Eric alisema.

Mchekeshaji huyo aliongeza kuwa kufanya hivyo kutakuwa sawa na kualika laana kwa kizazi chake.

“Fedha ni za aina nyingi sana, kuna damu, kuna mtu anaua ili apate fedha, halafu kuna mtu anafanya kazi kwa bidii ili apate fedha. Eric Omondi anafanya kazi kwa bidii ili kupata mapato yake. Sitawahi kutumia pesa hizo kujinufaisha.”

Kauli ya Eric Omondi ilikuja baada ya kukataa kuwasaidia  Magix Enga na mwana mteule ambao walihitaji msaada wa fedha.