Sikuenda shule hata kidogo, leo hii naimba Kiingereza shukrani kwa maEx wangu - Harmonize

“Ukiwa unasikiliza ngoma yangu yoyote ya Kiingereza, usipoelewa neno tatizo ni lako, rudini shuleni. Walimu wangu Sara na Briana saluti sana,," alisema.

Muhtasari

• Kwa sasa, Harmonize anajiliwaza kifuani mwa mrembo Poshy Queen ambaye inasemekana amemkwapua kutoka kwa aliyekuwa DJ wake, kwa jina DJ Seven.

Sarah Michelotti na Briana
Harmonize na wapenzi wake wa zamani// Sarah Michelotti na Briana
Image: Maktaba

Msanii wa Bongo Fleva Harmonize amewashukuru waliokuwa wapenzi wake wenye asili ya Ulaya na Australia, Sarah Michelotti na Briana kwa ufasaha wake katika lugha ya Kiingereza.

Msanii huyo alifunguka haya baada ya kuachia wimbo wake ambao alimshirikisha rapa wa Marekani Bobby Shmurda na msanii wa Kenya, Bien Aime Baraza – I Made It- wimbo ambao wameuimba kwa lugha ya Kiingereza.

Harmonize alijisikiliza jinsi alivyoweza kutema madini kwa lugha hiyo ya kigeni na kukumbuka kwamba si kwa uwezo au ujanja wake bali ni kutokana na mchango mkubwa kutoka kwa wapenzi wake wa zamani ambao waligeuka kuwa walimu wake kumpa mafunzo ya Kiingereza.

 Msanii huyo mmiliki wa lebo ya Konde Music Worldwide alifichua kwamba hakuweza kuhudhuria masomo hata kidogo lakini leo hii anabwabwaja kiingereza kama mtu mwenye digrii zake kadhaa.

“Ndio! Nakumbuka jinsi nilikuwa siwezi kuzungumza Kiingereza hata kidogo. Maisha ni kitu cha ajabu sana, sikuweza kwenda shule hata kidogo, lakini sasa hii ni lugha yangu,” Harmonize alisema.

“Ukiwa unasikiliza ngoma yangu yoyote ya Kiingereza, usipoelewa neno tatizo ni lako, rudini shuleni. Walimu wangu Sara na Briana saluti sana, leo hii tunafanya ngoma za kusikilizwa dunia nzima,” alimaliza.

Harmonize baada ya kuondoka lebo ya utotoni, WCB Wasafi, wengi wanahisi alijitafuta na kujipata kimaisha kutokana na msaada mkubwa kutoka kwa mpenzi wake kipindi hicho, Sarah Michelotti, raia wa Italia.

 Hata hivyo, baadae kuliibuka shtuma za kumsaliti kimapenzi kupelekea yeye kuondoka na baada ya muda akaonekana na mrembo kutoka Australia, Briana.

 Penzi lake na Briana halikuweza kudumu kwa muda kwani waliachana katika njia ya kisiri kabla ya kuibukia kwa muigizaji Kajala Masanja ambaye pia walitengana mwishoni mwa mwaka 2022 baada ya kuvishana pete za uchumba miezi sita nyuma.

Kwa sasa, Harmonize anajiliwaza kifuani mwa mrembo Poshy Queen ambaye inasemekana amemkwapua kutoka kwa aliyekuwa DJ wake, kwa jina DJ Seven.