Kama mumeo anakutesa tafuta mubaba wakikutana waligane, mshindi ndio wako! - Wolper ashauri

Alisema ikitokea mume wako amekufumania na mchepuko wako, basi kaa kando kama refa, waache wao wapigane na atakayeshinda mshike mkono nenda naye kwake kwani huyo ndiye wako halali.

Muhtasari

•   Kwa wale ambao tayari wameshaipata ndoa, Wolper aliwataka kutojitesa moyo bure kama wanaona wananyanyasika kwenye ndoa zao.

Image: Insta

Muigizaji mkongwe wa Bongo Movie Jackline Wolper ametoa ushauri wenye utata kwa kina dada ambao wanaifukuzia ndoa.

Wolper anahoji kwamba kwa wale ambao wanataka ndoa, basi wakiipata na waje kugundua kwamba wanaume wao hawawaheshimu na wanawatesa, basi wana kila haki ya kutafuta mwanamume aliyesonga kiumri kwa ajili ya kuwaliwaza.

Pia alishauri kwamba katika ndoa wakigundua mume wao ni mtu mnyanyasaji, wanafaa kuombea uzao wao ili wasije wakazaa watoto wenye tabia za baba.

"Mdogo wangu ambaye bado haujaingia kwenye ndoa usiombe Mungu kupata ndoa, omba Mungu akupe mume bora mwenye kukuheshimu na kukuheshimisha, usiombe tu kuolewa!!”

“Omba mume utakayempata asikutie aibu kila kukicha. Pia ombea uzao wake kama umezaa nae wanao wasiwe na tabia za uliyezaa nae ili hao wanao ndio wakawe faraja yako, ombea tumbo lako, sichekeshi nakukumbusha tu," alishauri mama huyo wa watoto wawili.

Kwa wale ambao tayari wameshaipata ndoa, Wolper aliwataka kutojitesa moyo bure kama wanaona wananyanyasika kwenye ndoa zao.

Aliwataka kutoka nje ya ndoa ili kumtafuta ‘mubaba’ wa kuwaliwaza pasi na kuhofia la kutokea iwapo mume halali atamfumania.

Alisema ikitokea mume wako amekufumania na mchepuko wako, basi kaa kando kama refa, waache wao wapigane na atakayeshinda mshike mkono nenda naye kwake kwani huyo ndiye wako halali.

"Lakini kama umeshaolewa na yakakukuta basi marufuku kulia, omba ku move on hapohapo kwenye ndoa kuwa na ndoa yako ya nje ili usife kwa stress za mtoto wa mtu uliyemkuta ukubwani na ndevu zake, kikubwa heshima tuu, wakikutana wapigane mshindi baki nae," Wolper alitoa ushauri.