“Kama mwanamume, kuna Baraka Mungu hawezi kukupa bila mke!” Mr Seed ashauri mabachela

“Kitu kimoja kizuri ambacho kiliwahi nifanyikiwa kutoka nizaliwe ni kuwa mzazi. Naweza sema ilikuja na Baraka nyingi, hapo ndipo niliona Baraka za kweli kabisa tena kwa macho yangu, zile Baraka unaona na unaweza gusa,” Mr Seed alisema.

Muhtasari

• Utakuwa bachela upate kila kitu unataka lakini kuna mahali Mungu hawezi fungua bila mke,'Mr Seed alisema.

• “Lakini vijana msioe haraka, stress zitawaua huku nje. Chukua muda wako kwa sababu ndoa si ya watu wa kufa moyo haraka.” aliongeza.

Mwimbaji Mr Seed amshukuru mke wake kwa kusalia naye na kumsaidia katika safari yake ya matibabu baada ya ajali mbaya ya barabarani.
Mwimbaji Mr Seed amshukuru mke wake kwa kusalia naye na kumsaidia katika safari yake ya matibabu baada ya ajali mbaya ya barabarani.
Image: INSTAGRAM

Msanii wa injili Mr Seed amefunguka jinsi hatua yake ya kumuoa mkewe Nimo Gachuiri ilikuja na Baraka tele, nyingine ambazo anahisi asingezipata akiwa mseja.

Katika mazungumzo kwa njia ya simu na kituo kimoja cha redio humu nchini, Mr Seed alisema kwamba mara yake ya kwanza kushuhudia na kuhisi kabisa kwamba amebarikiwa ni alipopandishwa cheo na kuitwa baba, baada ya kupata kifungua mimba wao.

“Kitu kimoja kizuri ambacho kiliwahi nifanyikiwa kutoka nizaliwe ni kuwa mzazi. Naweza sema ilikuja na Baraka nyingi, hapo ndipo niliona Baraka za kweli kabisa tena kwa macho yangu, zile Baraka unaona na unaweza gusa,” Mr Seed alisema.

“Ushaona tu kuna milango ilikuwa imefungika kwa maisha yako, halafu ukishachukua tu hiyo hatua ya kuoa, na ghafla kila kitu kinaanza kufunguka na kujipa kwa faida yako tu. Na ujio wa mtoto umekuwa ni safari nzuri na ya ajabu, unajua mimi sikulelewa na baba kwa hiyo ninajaribu pia kujifunza,” aliongeza.

Msanii huyo aliwashangaza watangazaji wa kipindi baada ya kuelezea Zaidi kwamba mara yake ya kwanza kununua ‘Christmas Tree’ nyumbani kwake, ni kutokana na mtoto wake, akielezea jinsi alikuwa na furaha kwani zamani akilelewa katika mtaa duni wa Mathare, alikuwa na kasumba kwamba ua zuri la krisimas hupatikana kwa nyumba za matajiri tu.

“Ujio wa mtoto wangu lilikuwa jambo la ajabu kiasi kwamba yeye ndiye alifanya Christmas tree yangu ya kwanza niliweka kwa nyumba yangu, ilikuwa inanifurahisha sana mpaka nilikuwa naambia kila mtu ‘waaah kwangu kuna Christmas tree’. Si unaelewa kulelewa huko Mathare unakua ukijua Christmas tree ni kwa nyumba za matajiri tu,” Mr Seed alisema.

Akizungumzia kuhusu Baraka zinazoambatana na ndoa, Mr Seed alisema kuwa Mungu anafanya kazi kwa njia ya ajabu kiasi kwamba kuna Baraka zingine ili mwanamume kuzipata, itabidi aoe kwanza, lakini akashauri dhidi ya kuoa kabla hujafanya maamuzi yako mwenyewe na ya kukuridhisha.

“Kwa maisha ya mwanamume, kuna Baraka ambazo Mungu hawezi kupa bila mke. Utakuwa bachela upate kila kitu unataka lakini kuna mahali Mungu hawezi fungua bila mke, kwa sababu Biblia inasema mkishaungana mnakuwa mwili mmoja. Mnafanya kazi kama timu.” Mr Seed alifunguka.

“Lakini vijana msioe haraka, stress zitawaua huku nje. Chukua muda wako kwa sababu ndoa si ya watu wa kufa moyo haraka.”