Chingiboy afichua kilichomchochea kumrudishia Stevo Simple Boy akaunti zake za mitandaoni

" Mambo yalitokea kadhaa na hasira pia zikapanda lakini nafikiri tulitafutana na nimeamua na roho yangu tumpe sapoti, niliona 150k si kitu kwangu,” Chingiboy alisema.

Muhtasari

• Katika kipindi hicho, Chingoboy alishikilia msimamo wake akidai kufidiwa kiasi cha laki moja na nusu kabla ya kuachilia akaunti.

Meneja wa zamani wa Stevo Simple Boy, Chingiboy Mstado ameelezea kwa undani sababu iliyomchochea kuanya uamuzi wa kumrudishia msanii huyo akaunti zake za mitandao ya kijamii baada ya kuvutaka kwa muda mrefu.

Wawili hao walikatisha uhusiano wao wa kufanya kazi yapata miezi mitatu iliyopita na wamekuwa wakizozana, Stevo akitaka kupatiwa uhuru wa kufikia na kusimamia akaunti zake ambazo zilikuwa mikononi mwa meneja Chingiboy.

Katika kipindi hicho, Chingoboy alishikilia msimamo wake akidai kufidiwa kiasi cha laki moja na nusu ambazo alitumia kuzikomboa akaunti hizo kabla ya kuziachilia kwa mtu ambaye alikuwa tayari kumuongoza msanii huyo, au hata kuziachilia kwa msanii huyo mwenyewe.

Hata hivyo, baada ya Stevo Simple Boy kuona kuwa hangeweza kupata kiasi cha pesa za fidia ambazo meneja alikuwa anadai kabla ya kuachilia akaunti, alifikia uamuzi wa kuanzisha akaunti zingine upya, kaitka kile kilichoonekana kama ishara ya kufa moyo ya harakati za ukombozi wa akaunti za awali.

Wiki moja kabla ya tangazo la kuanza upya, Chingiboy alifanya uamuzi wa kushtukisha kutangaza kukutana na msanii huyo na kuweka wazi kwamba amezika tofauti naye na kuzikabidhi akaunti zake kwake.

“Ni siku nyingi tangu tukae tusemezane hivi lakini nimefurahia kumuona tena, mambo yalitokea kadhaa na hasira pia zikapanda lakini nafikiri tulitafutana na nimeamua na roho yangu tumpe sapoti, niliona 150k si kitu kwangu,” Chingiboy alisema.

Kuhusu sababu ya kubadili msimamo na kutaka kuzirudisha akaunti zake, Chingiboy alifichua kwa mwandishi wa Makala haya kwamba aliona msanii huyo angekuja kusumbuka huko mbeleni akidai kuwa akaunti mpya zilizodaiwa kufunguliwa pia zilikuwa ni kupitia kwa mtu mwingine.

“Niliona boys atanyanyswa juu hata new accounts hazikufunguliwa na details zake,” Chingiboy alieleza.