Bunny Asila aeleza sababu ya kujitolea kusaidia watoto waliokuwa wakitaka msaada wake

“Mungu alitumia muziki kubadili maisha yangu na ya watu walionizunguka. Ndio maana huwa natamani niweze kusaidia talanta kila ninapokuwa katika nafasi. Kwa sababu ninaelewa kile inaweza kufanya na malezi sahihi.”

Bunny Asila ajitolea kusaidia msichana mmoja kati y kundi linaloimba nyimbo zake
Bunny Asila ajitolea kusaidia msichana mmoja kati y kundi linaloimba nyimbo zake
Image: Hisani

Bunny Asila, msanii wa injili Mkenya anayeishi nchini Finland amegusa nyoyo za wengi baada ya hatua yake ya kutaka kumsaidia mmoja kati ya watoto ambao wamekuwa wakitrend katika mitandao ya kijamii kutokana na uhodari wao katika kuimba.

Katika mtandao wa TikTok, mtumizi kwa jina Nyar Awendo amekuwa akipakia video za watoto hao watatu, mabinti ambao wanaonekana katika hali ya maisha duni wakitia jitihada zao katika kuimba baadhi ya tungo za injili.

Katika video hizo, watoto hao walikuwa wanatoa wito kwa Bunny Asila, lengo likiwa ni kupata usikivu wake na kuona jinsi atawasaidia kutusua katika maisha ya muziki wa injili.

“Bunny Asila, popote ulipo tunaomba utusapoti,” mmoja wao alisema katika video moja kabla ya kuanza kuimba wimbo wa Asila alioshirikishwa na Christina Shusho miezi minane iliyopita kwa jina ‘Nakuja”.

Katika video hizo, watoto hao wamekuwa wakifanya majaribio ya kupigiwa mfano kuimba baadhi ya nyimbo za Asila zikiwemo, Rafiki Pesa, Nakuja, miongoni mwa zingine katika ustadi wa kipekee.

Habari njema ni kwamba hatimaye video hizo pamoja na wito wa mabinti hao umemfikia Bunny Asila na ametoa tamko lake la ahadi ya kusaidia mmoja kati ya wasichana hao watatu.

Katika ujumbe wake kupitia kurasa zake kwenye mitandao ya kijamii akiwa mjini Helsinki nchini Ufini, Bunny Asila aliweka wazi kwamba video hizo zilimgusa moyo na kusema yuko tayari kubadilisha maisha ya mmoja wa watoto hao kutoka muziki hadi kielimu.

Sababu ya kujitolea mia fil mia kufanya hivyo, Asila alisema kutokana na mazingira ya wasichana hao, moja kwa moja yanamkumbusha maisha dunia ambayo alikulia enzi za utoto wake kabla ya muziki wa injili kumpaisha kwenda Ulaya.

“Hivi majuzi, nilitumiwa video za wasichana hawa wa ajabu ambao wamekuwa wakinitafuta na kutaka usaidizi wangu. Na sasa baada ya kujadiliana na timu yangu, tumeamua kumuunga mkono mmoja wao, hii ni kwa sababu hadithi yangu haina chochote zaidi ya kufanana na yao. Kwa hivyo baada ya kuomba na kufikiria juu ya hili, nimeamua kuchukua mmoja wao na kubadilisha maisha yake. Nimefanya hivi na watu wengi na hii haitakuwa mpya.” Asila alisema.

Msanii huyo aliyebatizwa kwa jina ‘Gospel One Europe’ na Cassypool baada ya kuifanikisha ziara yake Ulaya, alisema kwamba kila anapokumbuka jinsi Mungu alimtoa mbali kupitia muziki wa injili, katu hatosita kumshika mkono yeyote mwenye kipaji cha kuimba injili pia.

“Mungu alitumia muziki kubadili maisha yangu na ya watu walionizunguka. Ndio maana huwa natamani niweze kusaidia talanta kila ninapokuwa katika nafasi. Kwa sababu ninaelewa kile inaweza kufanya na malezi sahihi.”

“Kwa hivyo kuwatazama wasichana hawa na historia yao, inanikumbusha hali yangu. Kitu pekee walichonacho kwa sasa ni zawadi ya uimbaji. Huenda wasiweze kupata kitu kingine chochote ikiwa ni pamoja na nguo, karo ya shule, chakula n.k. Lakini wana muziki wenye njaa nyingi ya fursa,” Asila alifafanua Zaidi.