Muigizaji wa Kenya mwenye makao yake nchini Mexico ambaye ni mshindi wa tuzo ya Oscars 2014, Lupita Nyong’o amewamiminia sifa vijana wa Gen Z kwa kujitokeza kwa idadi kubwa kushiriki maandamano Jumanne.
Kupitia kurasa zake katika mitandao ya kijamii, Nyong’o alitoa hongera kwa vijana akisema kwamab walichokifanya kuonesha mshikamano na umoja dhidi ya muswada tatanishi wa fedha wa mwaka huu ni mfano wa kuigwa na vijana wengine wengi.
“Ninawapigia saluti vijana wa Kenya na ninawaonea fahari kwa jinsi walijitokeza kwa njia ya ajabu kupinga muswada wa fedha wa 2024 pamoja pia na kutetea haki ya kidemokrasia ya watu wa Kenya,” Lupita alisema.
Binti huyo wa gavana wa jimbo la Kisumu, Anyang’ Nyong’o aidha alionesha kutofurahia kwake kwa jinsi waandamanaji wasio na silaha waipoteza maisha yao mikononi mwa maafisa wa polisi waliokuwa wakijaribu kuwazuia wasiingie katika majengo ya bunge.
Binti Nyong’o aliitaka serikali ya Kenya kutafuta njia mwafaka za kuthibiti hali na wala si kumwaga damu za vijana wasio na silaha.
“Nimekasirishwa sana kwamba katika mchakato huo, maisha yalipotezwa na ninasimama na familia za walioathirika. Naomba serikali ya Kenya kulenga katika kuliunganisha taifa kwa njia ya Amani kwa kuwasiiliza vijana kuhusu uongozi,” aliongeza.
Lupita Nyong’o alimaliza kwa kuweka wazi msimamo wake kwamba anasimama na watu wengi kupinga muswada huo wa fedha.