Diamond Platnumz: Msanii wa kwanza chini ya jangwa la Sahara kufikisha wafuasi 9m YouTube

Diamond amefikisha idadi hiyo ya milioni 9 wikendi iliyopita na kusherehekewa na lebo anayoimiliki ya WCB Wasafi.

Muhtasari

• Diamond amefikisha idadi hiyo ya milioni 9 wikendi iliyopita na kusherehekewa na lebo anayoimiliki ya WCB Wasafi.

Diamond Platnumz amezidi kutamba na kujihakikishia nafasi yake katika Sanaa ya muziki barani Afrika.

Msanii huyo ambaye kwa sasa anazidi kuhanikiza katika mataifa ya bara Uropa kwa kibao chake cha Komasava ameweka rekodi nyingine ya kuwa mtu wa kwanza chini ya jangwa la Sahara kufikisha wafuasi milioni 9 kwenye YouTube.

Diamond amefikisha idadi hiyo ya milioni 9 wikendi iliyopita na kusherehekewa na lebo anayoimiliki ya WCB Wasafi.

Katika ukanda wa chini ya jangwa la Sahara, Diamond anaongoza kwa wafuasi milioni 9 huku akifuatiwa kwa umbali na Rayvanny mwenye wafuasi milioni 5.11, Burna Boy wa Nigeria akiwa wa tatu na wafuasi milioni 4.85, Harmonize na milioni 4.56, huku Fally Ipupa kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo akifunga tano bora kwa wafuasi milioni 4.24.

Wengine ni pamoja na Rema, Davido, Ckay wote kutoka Nigeria wakiwa na milioni 4.18, 4.02 na 4.02 mtawalia huku mshindi wa tuzo ya Grammy kutoka Afrika Kusin, Tyla akiwa wa tisa na wafuasi milioni 3.9 na Mr Flavour wa Nigeria akifunga kumi bora na wafuasi milioni 3.36.

Kwa upande wa Tanzania, Diamond anaongoza orodha hiyo kwa wafuasi milioni 9, akifuatiwa na Rayvanny, Harmonize, kisha Zuchu na milioni 3.32, Mbosso na wafuasi milioni 2.74, Alikiba na milioni 1.87, Lavalava na milioni 1.43, Nandy na wafuasi milioni 1.41, Marioo na milioni 1.33 kisha Rose Muhando akifunga kumi bora na akiwa msanii pekee wa injili na wafuasi milioni 1.24.