Pasta Ng’ang’a aorodhesha baadhi ya biashara anazomiliki, ‘sitegemei sadaka yenu!’

“Mimi siko hapa kwa sababu ya pesa, niko hapa nikuletee injili. Mimi si pasta eti nileteeni 2k ndio nikutabirie, kama hutaki kutoa wachana nayo, ukisikia kumtolea mtolee, kama hutaki kaa na pesa yako ununue Panadol,” alisema.

Muhtasari

• Ng’ang’a pia alidadavua baadhi ya fedha ndefu ambazo ametumia katika kuweka matangazo yake ya mkutano huo wa injili kwenye vyombo vya habari.

• “Ukiangalia hili bango hapa ni la thamani ya Ksh 168k, niliweka tangazo kwenye runinga ya Citizen, Ksh 250k na pia runinga ya Inooro Ksh 116k, nikatangaza pia na runinga ya NTV, Ksh 200k," aisema

PASTA NG'ANG'A
PASTA NG'ANG'A
Image: Sasa tv twitter X

Mchungaji James Ng’ang’a ameelezea sababu ya kuwachukia watu wanaojitambua kwamba wameokoka sana.

Kwa mujibu wa mchungaji huyo wa kanisa la Neno Evangelism, watu wengi wanaosema ni waokovu wengi wao ni wavivu, na yeye hapendi kujihusisha na uvivu kwani ni mjasiriamali mkubwa.

Akihubiri katika mkutano mkuu wa injili ulioandaliwa na kanisa lake mjini Kitengela wikendi iliyopita, Ng’ang’a aliorodhesha baadhi ya biashara nyingi anazomiliki, akisema kwamba hategemei sadaka na matoleo ya waumini.

“Mimi sipendi waokovu, sababu ni watu wavivu. Waokovu ni watu wa kutaka tu kutabiriwa, unatabiriwa nini? Mimi nilianza na mkokoteni kuuza matunda, nikapata baiskeli nikakwea hizo ngazi, sasa hivi waokovu wanataka tu kuomba omba,” Ng’ang’a alisema.

“Usinione hivi, umewahi niona nikikuambia mambo ya sadaka eti wapendwa mtolee Mungu? Msimtolee, kama humjui wachana naye. Mimi niko na hoteli, sasa hivi nimelima ekari karibu 60 za mahindi, niko na kituo cha petroli, niko na saluni na nataka pia kufungua kituo cha kuosha magari. Usinione mimi ni pasta tu, eti wapendwa wandugu…niko na matatu zangu pia na niko na nyumba zangu watu wanalala wananilipa, usifikirie mimi hapa ni kuwahubiria, jishughulishe na biashara zako,” mchungaji huyo aliongeza.

Ng’ang’a pia alidadavua baadhi ya fedha ndefu ambazo ametumia katika kuweka matangazo yake ya mkutano huo wa injili kwenye vyombo vya habari.

“Ukiangalia hili bango hapa ni la thamani ya Ksh 168k, niliweka tangazo kwenye runinga ya Citizen, Ksh 250k na pia runinga ya Inooro Ksh 116k, nikatangaza pia na runinga ya NTV, Ksh 200k, hesabu ni ngapi hizo? Unafikiri hapa zinaweza zikarudi? Hata hiyo mtatoa haiwezi fika hata 20k. Mimi siko hapa kwa sababu ya pesa, ukiondoka tu Mungu wangu anakuja,” alisema.

“Niko hapa nikuletee injili maana aliyeniombea mimi sikumpa kitu. Mimi si pasta eti nileteeni 2k ndio nikutabirie, eti mkuje mnione uso kwa uso ndio mniambie, kama hutaki kutoa wachana nayo, ukisikia kumtolea mtolee, kama hutaki kaa na pesa yako ununue Panadol,” aliongeza akisema amekasirishwa bure.