Akothee kurejea katika uimbaji wa muziki 2027 baada ya kuchukua likizo

Kutokana na kazi zake za muziki, mama huyo wa watoto 5 amefanikiwa kujijengea himaya ya kipekee na pia kuanzisha kampuni yake ya usafiri wa watalii na pia kukumbatia na chapa nyingi kama balozi wa mauzo.

Muhtasari

• Aliwataka mashabiki wake kuendelea kujiburudisha na kazi zake za awali za muziki, akiahidi kuwa urejeo wake mwaka 2027 utakuwa mkubwa, wa kipekee na kwa njia isiyotarajiwa.

AKOTHEE.
AKOTHEE.
Image: FACEBOOK

Msanii na mjasiriamali Esther Akoth maarufu kama Akothee amefichua sababu ya kimya chake cha muda mrefu katika Sanaa yake ya muziki.

Kupitia kurasa zake kwenye mitandao ya kijamii, Akothee amekiri kwamba ni kweli hajakuwa akifanya muziki kwa muda sasa lakini akasema kwamba hilo halimaanishi alistaafu kutoka Sanaa hiyo iliyomfungulia njia nyingi za mafanikio ya chapa yake.

Akitetea kimya chake kirefu kwenye muziki, Akothee alisema kwamba ni vyema mtu ukishajenga taaluma yake, unafaa kuitumia taaluma hiyo kujikuza na kujiimarisha katika sekta zingine.

“Kwa wale wanaojiuliza ikiwa nimeacha kuimba: kila kitu kina wakati wake. Unajenga taaluma kwanza, kisha uinue kazi hiyo ili kukuza uwezo wako mwingine,” Akothee alisema.

Akothee alisema kwamba kwa sasa yuko darasani akijifunza kuhusu kujikuza mwenyewe na atarejea kwa nguvu zote katika muziki mwaka 2027.

Aliwataka mashabiki wake kuendelea kujiburudisha na kazi zake za awali za muziki, akiahidi kuwa urejeo wake mwaka 2027 utakuwa mkubwa, wa kipekee na kwa njia isiyotarajiwa.

“Kwa sasa nimerejea darasani kwa ajili ya ukuaji wangu binafsi, lakini nitarudi na muziki mwaka wa 2027. Wakati huo huo jiandikishe kwa chaneli yangu ya YouTube na ufurahie TBTS. Hasa Albamu yangu ya Sibuor Madhako,” alisema.

Akothee ni mmoja kati ya wasanii wachache wa kike kutoboa tundu katika Sanaa ya muziki wa Kenya ambayo kwa asilimia kubwa inatawaliwa na wasanii wa kiume.

Kutokana na kazi zake za muziki, mama huyo wa watoto 5 amefanikiwa kujijengea himaya ya kipekee na pia kuanzisha kampuni yake ya usafiri wa watalii na pia kukumbatia na chapa nyingi kama balozi wa mauzo.

Pia ameweza kuanzisha shule yake ya kutoa elimu kwa watoto kutoka jamii zisizojiweza akisema kwamba hatua hiyo ilichochea na ugumu aliopitia katika maisha yake ya utotoni kutafuta elimu, ambayo mwisho wa siku amekuja kufuzu kutoka chuo kikuu baada ya zaidi ya miaka 14.