Baba T amwaga maua eneo la barabara ilikotokea ajali iliyomuua mkewe miaka 4 iliyopita

"Wakati mtu unayempenda anageuka kuwa kumbukumbu, hiyo kumbukumbu hugeuka na kuwa hazina kuu ya milele," alisema.

Muhtasari

• Akinukuu picha hiyo, alisema kwamba alikuwa amezama kwenye lindi la mawazo akimwaza mwenzi wake.

Image: Instagram

Tiktoker Baba Talisha ameendeleza msururu wa kumkumbuka na kumuenzi marehemu mpenziwe aliyefariki katika ajali ya barabarani.

Baba Talisha, jina halisi Faustine Lipuku Lukale alianza kuchapisha jumbe za kumuenzi na kumkumbuka mkewe wiki jana, ikiwa ni wakati kamili ambao alifariki miaka 4 iliyopita.

Baada ya kuchapisha ujumbe wenye hisia akimkumbuka, wikendi hii ametembelea eneo ajali iliyogharimu maisha yake ilitokea.

Baba huyo wa binti mmoja apiyeachia na marehemu mpenziwe alionekana kwenye video akiwa amebeba shada la maua akitembea pembezo mwa barabara hiyo giza likiwa linaingia.

Baada ya kufika katika eneo ambako ajali ilitokea akiwa na mpenziwe na mwanao ndani ya gari, Baba T alichuma maua hayo moja baada ya jingine na kuyadondosha kwenye barabara.

"Kwa yeyote anayebeba moyo mzito wa majonzi, kwa yeyote aliyempoteza mpendwa wake kwenye ajali ya barabarani, siku angavu ziko mbele," alinukuu video hiyo.

Kabla ya ziara hiyo kwenda eneo la tukio la ajali, Baba T alikuwa amechapisha picha angavu akiwa ameketi na kushika tama na mkono mmoja huku mkono mwingine ukiwa umeshikilia shada hilo la maua.

Akinukuu picha hiyo, alisema kwamba alikuwa amezama kwenye lindi la mawazo akimwaza mwenzi wake.

"Wakati mtu unayempenda anageuka kuwa kumbukumbu,  hiyo kumbukumbu hugeuka na kuwa hazina kuu ya milele," alisema.