Nilishangaa Afrika Kusini hakuna mtu ananijua kwamba mimi ni msanii – D Voice

“Nilikutana na watu ikabidi sasa nianze kujielezea baada ya kugundua kwamba kumbe kule mimi ni chipukizi" alisema.

Muhtasari

• Dvoice alikwenda Afrika Kusini wiki mbili akiwa ameandamana na Diamond Platnumz kwa ajili ya kusherehekea siku ya kuzaliwa ya bintiye, Tiffah Dangote.

DVOICE
DVOICE
Image: HISANI

Msanii wa lebo ya WCB Wasafi, Dvoice amewashangaza wengi baada ya kufichua ukweli mchungu uliomzaba kofi wakati akiwa Afrika Kusini na bosi wake.

Dvoice alikwenda Afrika Kusini wiki mbili akiwa ameandamana na Diamond Platnumz kwa ajili ya kusherehekea siku ya kuzaliwa ya bintiye, Tiffah Dangote.

Msanii huyo chipukizi alisema kwamba walipotua Afrika Kusini, kila mtu alikuwa anamrukia Diamond akitaka picha naye huku kwa upande wake kila mtu alikuwa anamuangalia na kumshangaa tu kama kituko.

Hata hivyo, alisema kwamba nchini Kenya alipata kutambulika angaa na mashabiki wachache.

“Safari yangu mimi kuenda Afrika Kusini na Diamond imenifafanuliwa vitu vingi ambavyo nilikuwa sivijui. Sisi tuliunganisha ndege tukashuka Nairobi kabla ya kuabiri nyingine kuelekea Afrika Kusini. Angalau kule Kenya nilizalimiwa na wadada kiasi lakini nilipofika Afrika Kusini, nilizalimiwa na mtu mmoja halafu wengine walikuwa wananiangalia kwa mshangao,” alisema.

“Mimi nilienda na Diamond kwenye mall kununua zawadi za wanawe, niligundua kama watu hawanijui, yaani nilizurura. Nimejifunza kwamba kuna angle bado hatujafikia kimuziki. Kwenye ile party, sijasikia wimbo hata mmoja wa wasanii wetu, hata kutoka WCB au Bongo kwa jumla,” msanii huyo alifunguka.

Alisema kwamba wimbo wa karibu zaidi anaoujua ambao aliusikia ni wa Mganda ambao umevuma wiki chache zilizopita, ‘Hozambee’.

“Nilikutana na watu ikabidi sasa nianze kujielezea baada ya kugundua kwamba kumbe kule mimi ni chipukizi. Ilinijia kwamba kuna wasanii wakubwa humu nchini ambao tukiwapeleka nchi kama Afrika Kusini hata viwanja hawajazi,” aliongeza.