“Nikiwa darasa la 8 tayari nilikuwa na kilo 100” – Willis Raburu

Raburu alisema kwamba suala la kukejeliwa lilikuwa linamsonga akili mara nyingi kwani kwa muda mrefu tu hakuwahi kupata ujasiri wa kujitazama kwenye kioo kuona mwili wake akiwa uchi.

Muhtasari

• “Nilianza kuumia kuhusu kukejeliwa tangu utotoni, na unajua wakati nikiwa mtoto, wakati nilikuwa darasa la nane, tayari nilikuwa na uzani wa kilo 100,” alisema.

WILLIS RABURU.
WILLIS RABURU.
Image: HISANI

Mtangazaji Willis Raburu amezungumzia historia ya kunyanyapaliwa kwake kutokana na uzani wa mwili wake.

Akizungumza kwenye podkasti ya mchekeshaji Dr Ofweneke, Raburu alifichua kwamba sababu iliyomfanya kutumia mchakato wa gastric bypass kupunguza uzito ni kutokana na kunyanyapaliwa kwa muda mrefu.

Mtangazaji huyo alisema kwamba safari yake ya kukejeliwa kuhusu uzani wa mwili wake haijaanza ukubwani bali ni jambo ambalo lilianza tangu akiwa mtoto.

Raburu alisema kwamba akiwa darasa la nane, tayari alikuwa na uzani wa kilo 100 na hivyo wanafunzi wenzake walikuwa wanamkejeli mara kwa mara.

“Nilianza kuumia kuhusu kukejeliwa tangu utotoni, na unajua wakati nikiwa mtoto, wakati nilikuwa darasa la nane, tayari nilikuwa na uzani wa kilo 100,” alisema.

“Siwezi sema kwamba nimeshazoea kejeli hizo lakini unajua siku hizo za utotoni, watu walikuwa wananikejeli kwa lugha ya Luo na kufikiri kwamba mimi si Mluo na hivyo sisikii kejeli zao, lakini nilikuwa nazisikia. Walikuwa wanasema ona vile huyu jamaa ni mnene, wananiita ‘Rao rabet’ kwa maana ya ‘mnyama kiboko mnene’. Na wakati huo niko darasa la na miaka kama 14,” Raburu aliongeza.

Raburu alisema alipitia kejeli hizo hadi wakati anaingia shule ya upili na hadi ukubwani alipojiunga na mitandao ya kijamii ambapo alikuwa akichapisha picha tu hivi watu wanaanza kumpa mzomo kuhusu uzani wa mwili wake.

Raburu alisema kwamba suala la kukejeliwa lilikuwa linamsonga akili mara nyingi kwani kwa muda mrefu tu hakuwahi kupata ujasiri wa kujitazama kwenye kioo kuona mwili wake akiwa uchi.

“Kwa muda mrefu singeweza kujitazama kwenye kioo nikiwa katika suti ya kuzaliwa. Singeweza. Sifikirii kuna wakati nilijiangalia kwa kioo nikiwa ile uchi kabisa. Kusema ukweli nilijiangalia kwa kioo kwa mara ya kwanza nikiwa uchi baada ya kufanya gastric bypass,” alifichua.