Christiano Ronaldo avunja rekodi ya YouTube dakika chache tu baada ya kufungua chaneli

Ndani ya saa 15, chaneli tayari ilikuwa imepata wafuasi zaidi ya milioni 13.

Muhtasari

•Christiano alifungua chaneli ya YouTube na ndani ya dakika chache tu alikuwa ameanza kupata wafuasi wengi kwenye jukwaa hilo.

•Ndani ya saa nne, chaneli yake mpya ilikuwa imefikia zaidi ya watu milioni nne waliojisajili.

Image: INSTAGRAM// CHRISTIANO

Mwanasoka matata wa Ureno Christian Ronaldo ameendelea kuvunja rekodi, sio tu uwanjani, bali pia hata kwenye majukwaa ya burudani.

Siku ya Jumatano, mshambulizi huyo mwenye umri wa miaka 39 alifungua chaneli ya YouTube na ndani ya dakika chache tu alikuwa ameanza kupata wafuasi wengi kwenye jukwaa hilo.

Christiano alifanikiwa kupata wafuasi  zaidi ya milioni moja katika dakika tisini za kwanza baada ya kufungua chaneli, rekodi ambayo haijawahi kuvunjwa hapo awali.

"Zawadi kwa familia yangu, Asante kwa SIUUUbscribers wote," Christiano alisema chini ya video yake akionyesha kibao cha dhahabu alichopokea kutoka YouTube baada ya kufikisha wafuasi  milioni waliojisajili.

Katika video hiyo, alionekana akisherehekea mafanikio hayo makubwa pamoja na familia yake na pia wakitazama huku mashabiki wengi wakiendelea kufuatilia channeli hiyo. 

Christiano alitangaza chaneli mpya ya YouTube siku ya Jumatano alasiri kupitiaakaunti zake za mitandao ya kijamii ambayo ina wafuasi wengi pia.

“Kuna nini jamani? nina surprise kwenu. Nina chaneli mpya ya YouTube, Nenda YouTube utafute URChristiano, na SIUUUbscribe” alisema kwenye video.

Jukwaa hilo jipya limeundwa ili kuwapa mashabiki mtazamo wa maisha ambayo nahodha huyo wa timu ya soka ya Ureno anaishi akiwa na mshirika wake Georgina Rodriguez.

Katika mojawapo ya video za kwanza, wanandoa hao wanafichua baadhi ya siri zao katika mchezo maarufu wa Bwana na Bibi.

Ronaldo pia anashiriki mambo kadhaa anayopenda kwenye video nyingine, na anatoa maoni yake kwenye NFL vs NBA, ndondi dhidi ya UFC na Rafa Nadal vs Novak Djokovic.

Ndani ya saa nne, chaneli yake mpya ilikuwa imefikia zaidi ya watu milioni nne waliojisajili.

Ndani ya saa 15, chaneli tayari ilikuwa imepata wafuasi zaidi ya milioni 13.