Shakib Lutaaya asherehekea ushindi wa mkewe, Zari Hassan kwa fahari

Mfanyibiashara huyo alimsifu Zari kwa bidii yake ya kufikia mafanikio na hatua kubwa alizopiga.

Muhtasari

•Shakib Cham Lutaaya amemsherehekea mke wake Zari Hassan kwa fahari baada ya kushinda tuzo maalum hivi majuzi.

"Jitihada zako zote hulipa kila wakati, Hongera kwa mafanikio na hatua zako," Shakib alimwambia Zari.

amemsherehekea mke wake Zari Hassan.
Shakib amemsherehekea mke wake Zari Hassan.
Image: INSTAGRAM// SHAKIB CHAM

Mfanyibiashara wa Uganda, Shakib Cham Lutaaya amemsherehekea mke wake Zari Hassan kwa fahari baada ya kushinda tuzo maalum hivi majuzi.

Mwishoni mwa wiki jana, mama huyo wa watoto watatu alitunukiwa tuzo ya Mhusika Bora wa Kike wa Runinga wakati wa Tuzo za Kitaifa za Afrika Kusini katika Filamu na Televisheni mwaka wa 2023z ilizofanyika katika Ukumbi wa Opera, jijini Pretoria mnamo Jumamosi, Oktoba 21.

Zari alitunukiwa tuzo hiyo kwa nafasi yake katika filamu maarufu ya Neflix ya Young, Famous na African.

“Usiku uliokuwa kwenye #NFTA National Film and Television Awards.. Asante kwa ‘jamii yangu’ kwa kupiga kura, asanteni Netflix na timu nzima. Hili lisingeweza kutokea bila nyinyi,” Zari alisema baada ya kushinda tuzo hiyo mwishoni mwa wiki.

Shakib ni miongoni mwa watu waliosherehekea hadharani sosholaiti huyo wa miaka 43 kwa mafanikio makubwa katika tasnia ya filamu.

Wakati akimsherehekea mkewe kupitia ukurasa wake wa Instagram, Shakib ambaye hivi karibuni alifunga ndoa rasmi na mpenzi huyo wa zamani wa Diamond Platnumz alimsifu kwa bidii yake ya kufikia mafanikio na hatua kubwa alizopiga.

"Jitihada zako zote hulipa kila wakati, Hongera kwa mafanikio na hatua zako," Shakib alimuandikia mkewe siku ya Jumanne jioni.

Wapenzi hao wawili kutoka Uganda walifunga ndoa rasmi katika harusi ya faragha iliyofanyika mnamo Oktoba 3, 2023  jijini Pretoria, Afrika Kusini baada ya kuchumbiana kwa zaidi ya mwaka mmoja.

Maelezo ya harusi hiyo yalikuwa yamefichwa sana lakini tulifanikiwa kupata baadhi ya picha na video za sherehe hiyo ya kukata na shoka.Picha hizo zilionyesha  Zari akiwa amevalia gauni la harusi refu jeupe huku Shakib akiwa amevalia suti ya kijivu na shati jeupe.

Baadhi ya wanafamilia wao wakiwemo watoto wa Zari; ; Pinto Tale, George Ssemwanga, Dido Ssemwanga Tiffah Dangote na Prince Nillan walikuwepo kwenye hafla hiyo. Tiffah alivalia gauni jeupe huku Prince Nillan akiwa amevalia suti ya kijivu na shati jeupe sawa na bi na bwana harusi.

Wana wa Zari na aliyekuwa mume wake, Ivan Ssemwanga walionekana wamevalia suti nyeupe, shati jeupe na viatu vyeupe. Wengi wa wageni waliokuwa wamealikwa kuhudhuria hafla hiyo walionekana wamevaa mavazi meupe. Wanaume walikuwa na suti ya kijivu wakati wanawake walivaa gauni za rangi ya dhahabu.

Video ilimuonyesha Shakib akisema viapo vya ndoa kisha kumvisha Zari pete kidoleni kabla ya wageni kupiga makofi kwa nguvu. Video nyingine iliwaonyesha wakiwa na watoto wa Zari wakipigwa picha ya familia huku wageni wakipiga makofi.

Mama yake Shakib pia alikuwepo kwenye sherehe hiyo.