logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Moto wateketeza mabweni mawili katika shule ya msingi Kisii na kuharibu mali ya mamilioni

Masanduku na vitabu vilivyokuwa vimeteketea vilitapakaa nje ya mabweni.

image
na

Yanayojiri18 May 2022 - 02:31

Muhtasari


•Hakuna mwanafunzi aliyejeruhiwa katika tukio hilo la usiku wa kuamkia Jumatatu huku mali ya mamilioni ya pesa ikiharibiwa.

•Masanduku na vitabu vilivyokuwa vimeteketea vilitapakaa nje ya mabweni wakati wanahabari walipowasili

Mzazi akibeba mabaki ya mali ya watoto wake wawili kutoka kwa vifusi katika shule ya bweni ya Sameta, Kisii Jumanne, Mei 17, 2022.

Moto mkubwa  uliteketeza mabweni mawili katika shule ya msingi ya Sameta, kaunti ya Kisii.

Hakuna mwanafunzi aliyejeruhiwa katika tukio hilo la usiku wa kuamkia Jumatatu huku mali ya mamilioni ya pesa ikiharibiwa.

Wanafunzi 82 waliokuwa wanalala katika mabweni yaliyoathiriwa waliweza kuponea bila majeraha.

Mwalimu mkuu Ibrahim Ondati hakuweza kubashiri kuhusu chanzo cha moto huo wakati wanahabari walipotembelea shule hiyo.

Bw Ondati hakuwepo shuleni wakati ambapo moto huo ulizuka mwendo wa saa moja usiku wa Jumatatu.

Aliwaelekeza waandishi wa habari kutembelea ofisi ya mkurugenzi wa elimu kwa maelezo zaidi.

Wazazi waliokuwa wamejawa na wasiwasi walisema walipokea simu wakifahamishwa kuhusu moto katika shule hiyo.

"Kila kitu katika eneo la tukio kimeharibiwa na moto kama unavyoona. Ni hasara kubwa lakini tuna furaha watoto wetu wako salama," alisema mama mmoja kwa mwanafunzi wa darasa la 7.

Masanduku na vitabu vilivyokuwa vimeteketea vilitapakaa nje ya mabweni wakati wanahabari walipowasili Jumanne alasiri.

Baadhi ya wazazi walionekana wakichukua watoto wao kwa magari.

Naibu Kamishna wa Kaunti ya Sameta Muroki Muyuri alisema ilikuwa bahati kuona hakuna mwanafunzi aliyejeruhiwa katika tukio hilo.

Hata hivyo wanafanya uchunguzi kubaini ikiwa mabweni yalichomwa na mtu. 

Moto huo ulizuka wakati hapakuwa na umeme shuleni, alisema.

"Tayari maafisa kutoka DCI wamezuru eneo la tukio na watafanyia kazi ripoti watakayotupa," alisema.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved