logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Mhubiri taabani kwa kuchoma miguu ya wavulana watatu kwa madai ya wizi wa keki

Mshukiwa alimpata mmoja kati ya wavulana hao watatu akiiba keki ya thamani ya Ksh 80.

image
na Radio Jambo

Habari26 May 2022 - 09:39

Muhtasari


•Mhubiri huyo alikamatwa pamoja na mshukiwa mwingine mmoja kuhusiana na madai ya kuchoma miguu ya wavulana watatu wanaodaiwa kuiba keki.

•Wavulana hao walilia kwa uchungu huku wakiomba kuhurumiwa ila washukiwa walikuwa wametia pamba kwenye masikio yao

Kanisa

Mhubiri  mmoja amejipata taabani baada ya kudaiwa  kutesa vijana watatu kwa kuiba keki katika duka la kuoka mikate mjini Kabarnet, kaunti ya Baringo.

Mhubiri huyo wa kanisa la Deliverance alikamatwa pamoja na mshukiwa mwingine mmoja kuhusiana na madai ya kuchoma miguu ya wavulana watatu wanaodaiwa kuiba keki.

Inaripotiwa kuwa mshukiwa alimpata mmoja kati ya wavulana hao watatu akiiba keki ya thamani ya Ksh 80 ndani ya duka hilo na kufahamisha wafanyikazi ambao walishirikiana naye kuchoma miguu yake kutumia jiko la kuoka mikate.

Huku wakiendelea kumtesa kwa moto washukiwa wanaripotiwa kulazimisha mvulana huyo kufichua majina ya washirika wake katika wizi wa keki.  

Baada ya kupatiwa majina ya wavulana mhubiri huyo aliandamana na wenzake hadi nyumbani kwao na kuwachukua kisha kuwapeleka kwenye duka lile la mikate ambapo walimpitishia mateso kama yale yale waliyofanyia mwenzao.

Wavulana hao walilia kwa uchungu huku wakiomba kuhurumiwa ila washukiwa walikuwa wametia pamba kwenye masikio yao.

Wakazi wa eneo hilo ambao walisikia vilio vya wahasiriwa waliingilia kati na kufahamisha polisi kuhusu yaliyotokea.

Mhubiri huyo na mwenzake walitiwa mbaroni na kupelekwa katika kituo cha polisi huku wakisubiri kufikishwa mahakamani.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved